Shein azindua uwanja wa Mao Tse Tung.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amekemea tabia iliojengeka nchini ya wanamichezo kupeleka kesi za michezo mahakamani, na kusema hatua hiyo imekuwa ikidumaza maendeleo ya michezo nchini  .

Dk. Shein aliyasema hayo jana katika hafla ya uzinduzi wa uwanja wa Mao Tse Tung uliopo Kikwajuni Mkoa wa Mjini Magharibi, ambao umejengwa kwa msaada wa serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kwa mashirikiano ya pamoja na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Alisema  michezo ni jambo la ridhaa na maelewano, hivyo matatizo yote yanayojitokeza, ni lazima yashughulikiwe na kumalizwa kwa busara.

Alitoa indhari kwa kubainisha kuwa kuanzia sasa hatokuwa tayari kusaidia shughuli za kimichezo, ikiwemo soka  endapo tabia ya kupeleka kesi hizo mahakamani itaendelea.

“Acheni tabia hiyo, mnaitia aibu nchi yetu, nataka nikwambieni kuwa FIFA inatuonea imani tu juu ya jambo hilo, ni matumaini yangu kuwa kesi za michezo hazitafikishwa tena mahakamani” alisema.

Aidha, Dk. Shein alisema serikali inakusudia kuongeza bajeti ya Wizara ya Vijana,Utamaduni, Sanaa na Michezo  kuanzia mwaka ujao wa fedha, ili kuimarisha na kuendeleeza michezo mbali mbali nchini.

Alisema hatua hiyo itakwenda sambamba na uimarishaji wa timu ya Taifa ya mpira wa miguu, ili kuleta ushindani na kuwa miongoni mwa timu bora katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Dk. Shein alieleza kuwa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  itahakikisha inafanikisha azma yake ya kujenga uwanja mkubwa wa kisasa utakaochukua watu 45,000 kutoka maeneo yaliyotengwa huko Fumba pamoja na Tunguu.

Katika hatua nyengine  Dk. Shein aliigiza Wizara ya Vijana,Utamaduni,Sanaa na michezo kuandaa programu nzuri itakayowezesha matumizi bora ya kiwanja hicho, ili uweze kudumu.

Alisema ni vyema kukawepo  utaratibu wa kuweka viingilio katika baadhi ya mashindano ili kuweza kupata fedha zitakazowezesha kukifanyia matengenzo madogo madogo kiwanja hicho pale panapohitajika.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa ujenzi wa uwanja huo ni utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020.

Nae Waziri wa Wizara ya Vijana, Sanaa, Utamaduni na Michezo Balozi Ali Abeid Karume alitoa shukurani na pongezi kwa Dk. Shein kwa jitihada zake za kuhakikisha uwanja huo unajengwa upya na una kuwa wa kisasa.

Balozi  Karume alimponmgeza Dk. Shein kwa kuweka kipaumbele suala la kuimarisha michezo, hivyo, akaahidi Wizara yake kuwaendeleza vijana pamoja na kukitunza ipasavyo kiwanja hicho.

Aidha, Balozi Karume alitumia fursa hiyo kueleza mafanikio na matunda ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964.

Nae Balozi Mdogo wa China anaefanya kazi zake hapa Zanzibar Xie Xiuowu alisema ujio wa mradi huo utaendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya China na Zanzibar.

Aidha, alisema kukamilika kwa kiwanja hicho pamoja na ujenzi wa viwanja mbali mbali vya michezo ya ndani (indoor games) kutaimarisha viwango vya wanamichezo wa Zanzibar na hivyo kufanya vyema katika mashindano mbali mbali.

Zanzibarleo.

Comments