NSSF Yaanza Kutekeleza Maagizo Ya Rais Dk.magufuli.

Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) limesema limeanza kutekeleza maelekezo ya Rais John Magufuli na wanachama wake watakaopoteza ajira kupewa mafao yao kulingana na utaratibu wa mfuko huo.

Taarifa ya NSSF kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana Januari 6,2019 imesema Mfuko unaendelea kupokea na kuhakiki madai mbali mbali kutoka kwa wanachama ambao ajira zao zimekoma na walikuwa kwenye ajira za muda maalumu kwenye sekta mbali mbali kama vile madini, viwanda, ujenzi na kilimo.

Imesema madai yote yanayothibitishwa kuwa ni halali baada ya kuhakikiwa, mwanachama atalipwa mafao yake.

Meneja Kiongozi wa Matekelezo (Chief Manager Compliance and Data Management ) Cosmas Sasi amesema NSSF inaendelea kulipa mafao mbali mbali kwa wanachama wake kwa wakati.

Amesema malipo hayo ni kwa watu ambao mikataba yao ni ya muda mfupi na ambao si rahisi kupata ajira nyingine baada ya kuachishwa.

"Kwa wanachama wetu ambao wanafanya kazi za muda mfupi kama ujenzi katika mradi fulani baada  ya mradi huo wanaweza kuchukua mafao yao, hata wale wenye ajira katika kampuni, ajira zao zikisitishwa watanufaika na utaratibu huu," alisema Sasi.

Alisema kwa watu ambao mikataba yao ya ajira inasitishwa lakini ni wataalamu na wana ujuzi fulani endapo watakuwa wamechangia kwa miezi 18 watapata pensheni ya kutokuwa na ajira kwa miezi sita ambayo ni theluthi moja ya mshahara waliokuwa wakipata, na baada ya hapo endapo itathibitika kuwa amekosa ajira atapewa mafao yake kwa mujibu wa taratibu za mfuko

Alisema utaratibu huu utawahusu wanachama ambao ajira zao zitakoma au watakaoachishwa kazi na si walioamua kuacha wenyewe na watalipwa baada ya mfuko kujiridhisha na hali zao za ajira kwamba kweli wamekosa kazi.

Kwa upande wa mafao ya uzeeni takribani Sh. bilioni 5 zimekuwa zinalipwa kila mwezi kwa wastaafu wetu kuanzia julai 2018.Wakati kwa pensheni ya Desemba,2018 Sh. Bilioni 4.83 zimeshalipwa kwa wastaafu 18,631 waolikuwepo kwenye daftari la wastaafu.

Kwa upande wa malimbikizo ya mafao hadi kufikia julai 2018 jumla ya Sh. bilioni 108 zilikuwa zinadaiwa kwenye Shirika, ambapo kiasi cha Sh. bilioni 85 kimelipwa kwa wanachama waliokuwa na madai mbali mbali baada ya uhakiki kukamilika, kiasi kilichobaki cha sh. bilioni 23 kitalipwa baada ya uhakiki unaondelea kukamilika.

Wakati huo huo Meneja Kiongozi Uhusiano na Elimu kwa UmaLulu Mengele alisema Mfuko ulianza mchakato wa kuhakiki wastaafu wake kuanzia Desemba 1, 2018 na bado unaendelea kwenye ofisi mbali mbali za NSSF zilizoko mikoa yote ya Tanzania Bara .

"Wastaafu ambao hawajajitokeza kuhakiki, wanaombwa wafike kwenye ofisi zetu 65 zilizoko katika maeneo mbali mbali katika mikoa yote Tanzania bara kwa upande wa wastaafu wanaoishi Zanzibar watahakikiwa kwenye ofisi za ZSSF.

"Wastaafu wanatakiwa kuwa na nyaraka zifuatazo picha, kitambulisho cha Taifa au cha mpiga kura pamoja na kadi ya benki," Alisema na kuongeza kwamba malipo ya pensheni kwa wastaafu ambao hawatahakikiwa yatasitishwa mwishoni mwa mwezi wa Januari 2019.

Mpekuzi.

Comments