KMKM,Malindi zapania kutinga fainali ya mapinduzi cup.

KOCHA mkuu wa timu KMKM Ame Msim,amesema kuwa wamejiandaa ili kuhakikisha wanafanya vyema katika mechi yao ambayo watacheza na timu ya Azam katika nusu fainali ya kombe la mapinduzi.

Alisema vijana wake wapo vizuri na wana ari kubwa sana ya mechi hiyo, kwani wamewajenga kisaikolojia ili kuhakikisha wanashinda mchezo huo na kutinga hatua ya fainali.

Alisema kuwa wanatambua kuwa mchezo huo utakuwa mgumu, lakini tayari wameisoma timu ya Azam na wanajua jinsi ya kuwakabili baada ya kubaini  mapungufu yao.

‘’Najua ni mchezo mgumu, ni mabingwa watetezi watahakikisha wanacheza ili kushinda na kujiweka nafasi nzuri ya kutetea ubingwa wao, lakini na sisi tumejipang ili kulitwaa taji hilo’’alisema.

Alisema mashirikiano ambayo yapo baina ya viongozi na wachezaji kwa kiasi kikubwa yanazidisha hamasa ya kuhakikisha mchezo huo wanaibuka na ushindi.

Kwa upande wake kocha msaidizi wa timu ya Malindi Ahmed Salehe Machupa,alisema mikakati yao ni kufanya vyema katika mechi yao na timu ya Simba ili kuhakikisha wanafikia malengo.

Alisema kuwa timu ya Simba ni timu kubwa lakini kwao wanaichulia ya kawaida, hivyo hana wasiwasi na watahakikisha wanacheza ka nguvu zote ili kushinda na kuingia fainali.

“Timu ya Simba ni kama timu nyengine na hakuna ambacho tunakiogopa kwao’’alisema.

Nusu hizo zitachezwa leo katika uwanja wa Amaan, ambapo majira ya saa 10:15 jioni  Azam itakipiga na KMKM na  saa 2:15 usiku Simba itakuwa uso kwa uso na Malindi.

Comments