Dk. Khalid ataka udhibiti mapato.

WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Khalid Salum Mohamed, amewataka watendaji wa serikali kuu na serikali za mitaa kuhakikisha kunakuwa na udhibiti wa mapato badala ya kuongeza vyanzo vipya.
Alisema kitendo cha kuongeza vyanzo vipya ni kuongeza mzigo kwa wananchi hivyo jambo la msingi ni kudhibiti mapato ya vyanzo vya sasa.

Akizungumza katika kikao cha kuibua mambo ya kuzingatia katika utayarishaji wa bajeti kuu ya mwaka 2019,2020 kilichowashirikisha watendaji wakuu wa serikali, serikali za mitaa na taasisi zinazohusiana na ukuaji wa uchumi kilichofanyika hoteli ya Ngalawa, alisema lengo la kikao hicho ni utekelezaji wa matakwa ya sheria namba 12 ya mwaka 2016 ambayo imetaka kuanzishwa kwa jukwaa la bajeti na uchumi.

Alifahamisha miongoni mwa maeneo yanayohitajika kupitiwa upya ni pamoja na hali ya uchumi, mfumo wa mapato, vyanzo vya mapato vinavyofanya kazi, matumizi ya fedha na changamoto zilizopo.

Pia alisema kutakuwa na utaratibu wa kuangalia sekta tatu zilizogatuliwa ikiwemo elimu, afya na kilimo ili kuhakikisha kunakuwa na urahisi wa upelekaji wa huduma za jamii na kufikia malengo ya serikali.

Alitaja eneo jengine ni uhaulishaji wa fedha kwa taasisi zilizogatuiliwa ambapo unapaswa kufanywa kwa kuzingatia vigezo ikiwemo idadi ya watu.

Sambamba na hilo, alisema eneo jengine litakaloangaliwa kwa umakini ni pamoja na hali ya umasikini katika utafiti wa kaya uliofanywa mwaka 2014 -2015.

Kuhusu rasilimali watu wenye ujuzi, alisema kamati maalumu imeundwa ya kuangalia eneo hilo na kupatiwa ufumbuzi sambamba na kamati ya kuangalia sheria na mahitaji ya fedha kulingana na mahitaji.

Alisisitiza misingi ya uadilifu na uwajibikaji wenye kuzingatia sheria za fedha na taratibu zilizopo katika vyanzo vya mapato ili kukuza kiwango cha ukusanyaji.

Nae Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Khamis Mussa Omar, alisema ugatuzi ni miongoni mwa eneo muhimu la kufanyiwa tathmini ya haraka na kuangalia changamoto zilizopo.

Alisema ugatuzi ni njia moja wapo ya kuharakisha upelekaji wa huduma za kijamii hivyo linahitaji kutekelezwa kwa weledi.

Nae Kamishna wa bajeti, Mwita Mgeni Mwita, alisema kikao hicho kinapokea michango, maoni na mapendekezo yatakayokusanywa na kuingizwa katika mkabala wa bajeti ambayo itapelekwa Baraza la Mapinduzi na Baraza la Wawakilishi kwa ajili ya kujadiliwa na kuridhiwa.

Mchangiaji kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania, Saleh Haji, alipendekeza kuandaliwa mfumo maalumu wenye kudhibiti mapato katika maeneo ya bandari bububu.

Comments