Balozi Seif ataka michezo itumike kupinga udhalilishaji

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amewakumbusha wanamichezo nchini kutumia nafasi yao kwa kuongeza mapambano dhidi ya  kupinga vitendo vya udhalilishaji vinavyoleta sura mbaya katika Jamii na Taifa kwa ujumla.

Alisema sekta ya michezo ina ushawishi mkubwa miongoni mwa Jamii  na inaweza kutumika vyema katika mapambano hayo, na kuleta mafanikio makubwa katika jitihada za kukabiliana na kadhia hiyo.

Balozi Seif Ali Iddi ametoa kumbusho hilo wakati akikabidhi zawadi kwa timu ya soka ya Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU) iliyotwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Zanzibar kwa Mwaka 2018/2019 na mshindi wa Pili timu ya Kikosi cha Zimamoto na Uokozi hafla iliyofanyika ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.

Vifaa hivyo vilivyoambatana na shilingi milioni 2,000,000/- kwa JKU na milioni 1,000,000/- kwa Zimamoto, vilivyotolewa na mdau wa michezo Mohamedraza Hassanaali ni pamoja na seti za jezi, viatu, mipira, pea 40 za viatu kwa timu ya wanawake ya mpira wa Pete ya JKU pamoja na seti ya jezi kwa timu zote za Vikosi vya SMZ.

Comments