Pembe, walimu wazungumzia uvujaji mitihani.

Image may contain: 4 people, people sitting and tableWAZIRI wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Riziki Pembe Juma, amesema wizara inaendelea kufanya uchunguzaji juu ya kuvuja kwa mitihani ya kidatu cha pili, iliyoanza Disemba 3 mwaka huu.

Aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na walimu wakuu, masheha, wajumbe wa kamati za skuli na viongozi kutoka mkoa wa mjini magharibi, katika skuli ya Haile selassie.

Alisema kwa sasa hawajajua sababu iliyosababisha kuvuja kwa mitihani wala kubaini aliyesababisha tatizo hilo.

“Hatuwezi kusema tunamtuhumu mtu ila tunachosema mazingira yamechangia kuvuja kwa mitihani hiyo na kusabisha hasara kubwa kwa serikali”, alisema.

Aidha aliiomba jamii kufahamu kuwa serikali imefanya jambo la haki la kusitisha mitihani hiyo kwa lengo la kuwajenga wanafunzi hao kielimu.

“Tungeruhusu mitihani iendelee wanafunzi wengi wengefaulu lakini mbele wangeshindwa la kufanya katika madarasa ya mengine, kuondokana na hilo tumeamua kupata hasara ili kutunga mitihani mengine,” alisema.

Pia aliwaomba walimu wakuu na kuwataka wanafunzi wao kurudi skuli ili kuendelea na masomo mpaka mitihani itapoanza tena.

“Tunaomba walimu wote wanaosomesha kidato cha pili kurudi skuli hata kama hawatasomesha kama mwanzo na i wanafunzi wanatakiwa kurudi na kufanya marudio katika masomo yao”, alisema.

Aidha aliwaomba masheha na wajumbe wa kamati za skuli kupitia skuli zao kuangalia wanafunzi na walimu kama wanafika skuli.

Nae Naibu wa wizara hiyo, Mmanga Mjengo Mjawiri, aliwaomba walimu kutojishirikisha na vitendo vya uvujishaji mitihani.

Nao walimu walioshiriki kikao hicho, waliiomba wizara hiyo kuangalia vizuri wachapishaji ili kujua wahusika wa tukio hilo.

Zanzibarleo.

Comments