Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Said Hassan Said, alieleza hayo ukumbi
wa Baraza la Wawakilishi Chukwani, wakati akitoa ufafanuzi kwa hoja
iliyowasilishwa na Mwakilishi wa jimbo la Kikwajuni, Nassor Salim Ali
(Jazira) juu ya kuunga mkono hatua ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kuingia katika mkataba wa ugawaji wa mafuta.
Alisema utiaji saini mkataba huo ulifanywa kwa sheria na kufuata kanuni, hivyo ni vyema wananchi kujua umuhimu wa mkataba huo.
Alisema wapo wananchi ambao wameanza kubeza mkataba huo baada ya
kupata taarifa kuwa mafuta yatakayopatikana yatakuwa ya mgao na Zanzibar
haitanufaika kwa asilimia kubwa.
Alisema wananchi wa Zanzibar watapata asilimia 70 ya mgao unaotokana
na raslimali hiyo na sio kugawiwa sawa sawa kama inavyodaiwa na baadhi
ya wananchi.
Aidha aliwaomba wajumbe wa Baraza la Wawakilishi pamoja na wananchi
kuacha kusikiliza propaganda za kupotosha juu ya mkataba huo.
Aliwahimiza wawakilishi kuzisoma sheria na kuacha kusikiliza maneno ya mitaani ya upotoshaji ambayo yana nia mbaya.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohammed Aboud
Mohammed, akifafanua juu ya hoja hiyo alisema wapo watu wanafanya kila
jitihada kuhakikisha wanakwamisha utafiti wa mafuta na gesi lakini
wameshindwa.
Alisema mapato ambayo yatapatikana katika sekta hiyo yatawasaidia
wananchi ambapo wazanzibari wameanza kunufaika tangu kutiwa saini
mkataba huo.
Mapema wakichangia hoja hiyo, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi,
walimuunga mkono Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,
Dk. Ali Mohamed Shein, kwa kutia saini mkataba wa mgawanyo wa uzalishaji
wa mafuta.
Walisema Dk. Shein anastahili kupongeza kutokana na kujali maslahi ya wananchi anaowaongoza.
Zanzibarleo.
Comments