Wagonjwa wa kisukari watakiwa kuacha kutumia dawa za asili.

MKURUGENZI Idara ya Kinga na Elimu ya Afya katika Wizara ya Afya, Dk. Fadhil Mohamed, amewaomba wananchi kuacha tabia ya kutumia dawa za miti shamba ambazo hazijathibitishwa na wataalamu ili kuepuka maradhi.

Akizungumza na Zanzibar Leo, alisema kuna baadhi ya wananchi hasa wagonjwa wa sukari wanatumia dawa za miti shamba hali ambayo inasababisha ugonjwa huo kuwa sugu.

Alisema dawa zisizo na  kiwango pia zinasababisha ongezeko la maradhi ambayo pia tiba yake kuipata inakuwa ni ya shida.

Alisema wagonjwa wengi wa sukari wanapata matatizo kutokana na kutumia  dawa za miti shamba ambazo hazijathibitishwa na wataalamu wa afya.

Hivyo aliwaomba kuacha tabia ya kutumia dawa za asili na pale wanapobidi basi watumie dawa zilizothibitishwa na wataalamu wa afya.

Alisema wizara itaendelea kutoa elimu ya afya kupitia vyombo vya habari kuhusu maradhi yasiyoambukiza ikiwemo kisukari pamoja na athari za matumizi ya dawa asili zisizothibitishwa.

Zanzibarleo.

Comments