Castico aifariji familia ya mtoto aliefariki wakati akicheza.

WAZIRI wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto, Maudline Castico, ameifariji familia ya mtoto wa miaka sita aliyefariki katika hospitali ya Mnazimmoja, baada ya kupigwa teke la tumbo na mwenzake wakati wakicheza.

Baba mzazi wa mtoto huyo, Juma Khamis, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo ambapo binti yake aliyefahamika kwa jina la Asfar Juma Khamis, alifariki baada ya kupigwa teke la tumbo na mwenzake.

Mazishi ya mtoto huyo, yalifanyika Mahonda wilaya ya Kaskazini B Unguja.

Alisema, tukio hilo lilitokea Jumamosi ambapo binti yake alirudi kutoka chuoni na kusema anaumwa homa na kulala hadi siku ya pili.

“Siku hiyo binti yangu hakushinda vizuri, ndipo tulipopata taarifa kwamba alipigana na mwenzake, usiku wa Jumatatu mwanangu alitapika sana usiku ndipo asubuhi tulimpeleka hospitali,” alisema.

Alisema hospitalini alilazwa kwa ajili ya matibabu zaidi lakini kwa bahati mbaya alifariki wakati akiendelea na matibabu.

Naye Waziri Castico wakati akiifariji familia hiyo, aliwaomba wazazi na walimu kuwafundisha watoto kucheza michezo mizuri isiyohatarisha maisha yao.

Aidha Castico aliitembelea familia ya mwanamke aliyefariki baada ya kupigwa rungu la kichwa na kusisitiza suala la upendo kwa familia.

Pia alipata nafasi kutembelea ofisi za Zan Tour kwa ajili ya kufuatilia masuala ya wafanyakazi na mazingira ya kazi kwa ujumla.

Zanzibarleo.

Comments