Castico alia na udhalilishaji wanawake mitandaoni.

WAZIRI wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto, Maudline Castico, amekemea vikali vitendo vya matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii.

Alisema hayo, kufuatia tukio la watu kusambaza katika mitandao ya kijamii picha za utupu za mwanafunzi wa kike, jambo ambalo ni udhalilishaji mkubwa wa kijinsia.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mwanakwerekwe, alisema, sheria lazima ifuate mkondo wake kwa watuhumiwa waliosambaza picha hizo katika mitandao ili iwe fundisho kwa wengine.

Aidha alisema tabia ya watu kusambaza mambo mabaya katika mitandao ya kijamii inaonekana kuendelea jambo ambalo halileti taswira nzuri katika vita dhidi ya udhalilishaji.

“Kuna mambo mengi ya maendeleo yanayofanywa na serikali, lakini jamii haiyatangazi, badala yake hutangaza mambo ambayo hayaleti picha nzuri katika jamii,” alisema.

“Unapomdhalilisha mtoto wakike basi unamdhalilisha kiongozi wa baadae, unamdhalilisha mke wa mtu na pia unamdhalilisha mama wa baadae” alifahamisha.

Alisema, mitandao ya kijamii imekuwa jaribio la kufanyiwa ukatili watoto hali ambayo inarudisha nyuma maendeleo ya watoto na kuathiri vizazi.

Aidha, alifahamisha kuwa, wizara watafuatilia suala hilo na kujua nani aliyesambaza picha hizo ili achukuliwe hatua za kisheria.

Sambamba na hilo, pia alisema, wiki ya mtoto wa kike duniani kilele chake kitakuwa Oktoba 11 ambapo na kauli mbiu kwa mwaka huu inasema ‘tumpe ujuzi mtoto wa kike kwa maendeleo endelevu’.

Aliwaomba wananchi kuacha muhali katika vita dhifi ya udhalilishaji na badala yake wawafichue watu wanaotenda vitendo hivyo hata kama ni jamaa zao.

Zanzibarleo.

Comments