Balozi Seif: Wanafunzi wasiozeshwe waume.

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idi, amewataka wazazi wa wilaya ya Micheweni, kuacha tabia ya kuwaozesha waume watoto wao wakati wakiwa wanafunzi.

Alisema hayo wakati akizungumza na wazazi, walimu na wananchi wa Maziwang’ombe, baada ya kuweka jiwe la msingi skuli ya maandalizi Maziwang’ombe.

Alisema elimu ndio kitu muhimu katika maisha ya kila mtu, hivyo lazima watoto wa kike wapatiwe elimu badala ya kuozeswa waume.

 “Hipendezi sisi wazazi kuwaozesha watoto wetu badala yake tuwaachie wasome, kwa ajili ya maisha yao ya baadae,” alisema.

Aidha aliwashauri walimu kutowatoza fedha wanafunzi, kwani serikali imejidhatiki kulipia gharama zote zinazowahusu wanafunzi wa msingi na sekondari.

Aidha alisema serikali imedhamiria kuwapatia elimu bora watoto, kwa kuanzia na ngazi za maandalizi hadi sekondari.

Alisema kujengwa kwa skuli ya maandalizi Maziwang’ombe, kutawahamasisha watoto kusoma kwa bidii na serikali kufikia malengo yake.

Akizungumzia skuli Micheweni, alisema serikali inaendelea kutoa fursa kwa wanafunzi kusoma mpaka kiwango wanachotaka, kwani fursa za kufanya hivyo zipo.

Alikemea kitendo kilichofanywa na baadhi ya wananchi kuzuia ujenzi wa ukuta wa chuo cha CCK Micheweni, huku akiutaka uongozi wa chuo hicho kujenga ukuta kwani ardhi ni mali ya serikali.

Akizungumza na walimu ambapo skuli zao zimefanya vizuri na kupata daraja la kwanza, alisema sasa umefika wakati wa kushindanisha mikoa ili kupasisha wanafunzi wengi wa kidato cha sita na nne.

“Naamiamini mikoa ya Pemba inaweza kufanya vizuri, mjini magharibi pia, hata mikoa yote itafanya vizuri, kazi kubwa mlionayo ni kuwasomesha vijana wetu,” alisema.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Riziki Pembe Juma, aliwaomba wafanyabiashara kujitokeza kusaidia sekta ya elimu, kama anavyofanya mfanyabiashara Said Nassir Nasoor (Bopar).

Zanzibarleo.

Comments