Magufuli atengua na kuteua watendaji wa wizara.

Rais John Magufuli amefanya uteuzi wa watendaji wawili akiwamo Dk John Jingu kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto anayeshughulikia Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
Taarifa iliyotolewa  leo jioni Septemba 3, 2018 Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu, imesema Dk Jingu alikuwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliyechukua nafasi ya Sihaba Nkinga ambaye uteuzi wake umeteuguliwa.
Pia, Rais Magufuli amemteua Gabriel Malata kuwa Kamishna wa Kazi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu.
Taarifa hiyo imesema kabla ya uteuzi huo, Malata alikuwa Mkurugenzi Msaidizi Kesi za Madai, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Malata amechukua nafasi ya Hilda Kabisa ambaye uteuzi wake umetenguliwa.

Comments