Wajawazito Wanatakiwa Kupata Huduma Za Uzazi Bure-dk. Ndugulile.

SERIKALI kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesisitiza kuwa huduma za uzazi kwa wajawazito zinatolewa bila ya malipo katima Hospitali na vituo vya afya vya Serikali.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile wakati wa ziara yake ya kujua hali ya utoaji wa huduma za afya katika Hospitali ya Rufaa Temeke, Amana na Mwananyamala leo jijini Dar es salaam.

“Nimesikia pale wajawazito wameniambia wamekuja na vifaa vya kujifungulia kutoka majumbani mwao sitaki kusikia mwanamke mjamzito analipishwa wala kuja vifaa vya kujifungulia kwani sera yetu inasema huduma za uzazi ni bure” alisema Dkt. Ndugulile.

Aidha Dkt. Ndugulile alisema kuwa wanawake wajawazito , watoto chini ya miaka 5 na wazee wasio na uwezo wanapata matibabu bure kulingana na sera ya Afya inavyosema. Mbali na hayo Dkt. Ndugulile amesema kuwa kila mtoa huduma anapaswa kuandika taarifa ya mgonjwa kabla na baada ya kumpa huduma katika kituo chake cha kazi.Aidha Dkt. Ndugulile aliwataka watoa dawa katika hospitali na vituo vya afya kuandika majina asilia ya dawa na siyo yale ya kampuni pamoja na kufuata muongozo wa dawa uliyowekwa na Serikali.

“Marufuku watoa dawa kuwaandikia wagonjwa dawa na kwenda kununua nje ya kituo cha afya na badala yake dawa zote zitolewe katika hospitali au kituo cha afya kama zimeisha zinatakiwa kuagizwa kwa haraka na nauagiza uongozi wa Hospitali ya Amana kuwarudishia wagonjwa wa wodi ya watoto waliokwenda kununua dawa nje leo hii ” alisema Dkt. Ndugulile.

Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa Temeke Dkt. Amaan Malima amesema kuwa changamoto kubwa inayowakumba ni upungufu wa watumishi .

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Hospitali ya Rufaa ya Amana Dkt. Meshack Shimwela amesema kuwa anaomba radhi kwa tatizo hilo lililojitokeza kwani hakuna tabia kama hiyo hospitalini hapo na amehaidi kulifanyia kazi haraka iwezekanavyo.
Mpekuzi.

Comments