Waziri Mkuu ashauri wajenzi wakope trilioni 1/- NEEC.

WAJENZI wametakiwa kutumia fursa ya uwepo mifuko 19 yenye ukwasi wa zaidi ya Sh trilioni 1.3 katika Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kitaifa (NEEC) kukopa ili kuimarisha, kuboresha, kuongeza bidhaa na kupanua huduma zao.

Akizindua Maonesho ya Wajenzi Dodoma kwa niaba ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, (Kazi, Vijana na Ajira), Anthony Mavunde alisema fursa hiyo ni muhimu kwao waitumie kwa kuinua mitaji na kuboresha bidhaa na huduma zao.

Maonesho hayo ya Wajenzi Dodoma ya siku mbili yenye kaulimbiu 'Tunajenga Jiji la Dodoma,' Majaliwa alisema wanatakiwa kutoogopa kutumia fursa hiyo ya uwepo wa mifuko hiyo katika kukopa na kupata fedha za mitaji katika kuzalisha bidhaa ambazo zitachangia kuboresha bidhaa za ujenzi wa Dodoma kuwa mji wa kisasa zaidi.

“Serikali ipo pamoja na kampuni za wazawa ambazo zinazalisha bidhaa na zinazoa huduma mbalimbali, hivyo nazo zinatakiwa kutengeneza bidhaa zenye viwango ili kuleta mchango katika uchumi nchini,” alisema.

Alisema kampuni hizo zikipata mikopo zitasaidia vijana ambao ni nguvukazi muhimu kupata kazi na kutoa mchango mkubwa katika kuzalisha bidhaa na kukuza uchumi na kufikia malengo ya kuwa na uchumi wa kati ifikapo 2025.

“Wajenzi watakuwa wamechangia kwenye mkakati wa serikali ambao unataka ifikapo 2021, vijana asilimia 40 wana kwenye shughuli za viwanda,” alisema Waziri Mkuu.

Alisema katika kufikia azma hiyo ya kuwa katika uchumi wa kati mwaka 2025, lazima kuwa na namba maalumu za vijana wenye ujuzi mkubwa ili kushiriki katika uzalishaji viwandani.

Alisema kwa sasa takwimu zinaonesha kwamba nchi ina nguvu kazi ya watu milioni 23.3 na vijana wenye umri wa kati ya miaka 14 hadi 34 ni milioni 14.4 ambao wanatakiwa ndio wanatakiwa kuwa kuwa na ujuzi ujuzi wa juu.

“Kwa sasa ni vigumu nchi kufikia katika uchumi wa kati kama vijana wengi wenye ujuzi wa juu, kati na chini ni wachache, hivyo inatakiwa kuongezeka ili kufikia malengo hayo.

Alisema kati ya nguvukazi hiyo ya vijana milioni 22.3, wenye ujuzi wa juu ni asilimia 3.6 tu, ujuzi wa kati ni asilimia 16.5 na ujuzi wa chini ni asilimia 79.9, kiwango ambacho ni kidogo.

“Ili kufikia uchumi wa kati inatakiwa kuwa vijana wenye ujuzi wa juu asilimia 12, wa kati asilimia 34 na wa chini asilimia 54," alisema.

Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Simon Odunga alisema lengo la maonesho hayo ni kuhakikisha watu wanapata fursa ya kwenda kuona maonesho ili kupata bidhaa zenye ubora kwa ajili ya ujenzi wa Dodoma.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Elias Kwandikwa alisema wajenzi wanatakiwa kuhakikisha wanazalisha bidhaa bora ambazo zitashindana katika soko la nje ya ndani ya nchni.

Majaliwa alisifia waandaaji wa maonesho hayo yanayoshirikisha kampuni 40, ambao ni Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) pamoja na AFM, akisema ndio yameanza, lakini baadaye yatakuwa makubwa na kushirikisha kampuni za nje ili kupata taaluma, mang'amuzi na ujuzi wao.
Mpekuzi.

Comments