Dk. Shein alieleza hayo jana ikulu mjini Zanzibar alipokutana na
uongozi wa wizara hiyo ilipowasilisha utekelezaji wa mpango kazi kwa
mwaka 2017/2018 na mpango kazi wa utekelezaji kwa mwaka 2018/2019.
Alisema kuna umuhimu wa kutangazwa mafanikio ya kiutendaji
yaliyofanikishwa na wizara hiyo kupitia vyombo vya habari. Nao kuongeza,
“Hakuna wa kuyasema mambo ya kilimo, mifugo, uvuvi na maliasili kama si
siye wenyewe, mmefanya mambo mengi mazuri”,alisisitiza.
Alifahamisha umuhimu wa kutolewa mafunzo kwa lengo la kuwaandaa
wataalamu watakaosadia kuimarisha sekta hizo ikiwa ni pamoja na
kuendeleza ufanyaji wa tafiti ambazo ndio nguzo muhimu kwa wizara hiyo.
Dk. Shein aliwakumbusha viongozi wa wizara hiyo umuhimu kwa viongozi
kuwa wasikivu na kukaribisha ushauri, kwani viongozi huwatumikia
wananchi hivyo ni vyema kusikilizwa matatizo yao na kuepuka kukaa
ofisini hasa kwa maumbile ya sekta hizo.
Aidha alieleza kuwa zoezi la bango kitita limeweza kufanikiwa kwa
kiasi kikubwa katika kuendeleza na kutekeleza mipango yote muhimu
inayopangwa na wizara za serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Awali waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Rashid Ali Juma
alieleza kuwa sekta ya kilimo ikijumuisha mazao ya mifugo, uvuvi na
misitu bado inaendelea kuwa ni muhimili mkuu wa uchumi wa Zanzibar.
Aidha, alieleza kuwa inakadiriwa kuwa zaidi ya asilimia 70 ya
wananchi wanategemea sekta hii ambayo imeongoza kwa ukuaji katika pato
la Taifa na kufikia wastani wa asilimia 8.8 mwaka 2017 kutoka ukuaji wa
wastani wa asilimia 3.6 wa mwaka 2016.
Aliongeza kuwa mwaka 2017 sekta ya kilimo imekuwa ya pili kuchangia
pato la taifa kwa wastani wa asilimia 27.9 ikilinganishwa na asilimia
25.5 mwaka 2016.
Zanzibarleo.
Comments