Askari Watatu Kizimbani kwa Kuomba Rushwa.

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) wilayani Chato mkoa wa Geita, imewafikisha mahakamani askari watatu wa hifadhi ya wanyamapori kwa makosa ya kuomba na kupokea rushwa.

Washtakiwa hao ni Flora David Ngowi, Agnes Paul Shokolo na Omary Mweya Mazanza pamoja na wakala wa M-pesa, Nicholaus Fortunatus Nyilala, kwa makosa ya kuomba na kupokea rushwa kinyume cha Kifungu cha 15 (1) (a) na (2) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11/2007.

Akiwasomea mashtaka hayo juzi mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Chato, Yona Charles Myombo, Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Augustino Mtaki, alidai kuwa Desemba 2, mwaka jana, washtakiwa wakiwa Wilaya ya Chato walimwomba Safari Masasi Sh. 9,000,000 ili wasitaifishe ng’ombe wake walioingizwa kwenye pori la akiba la Biharamulo.

Mwendesha mashtaka huyo aliendelea kudai kuwa siku hiyo hiyo, 2/12/2017 Nicholaus Fortunatus Nyilala alipokea fedha za rushwa Sh. 9,000,000 kwa niaba ya wenzake kutoka kwa Masasi kwa njia ya M-pesa,

Aidha, ilidaiwa Desemba 3, 2017, kwa nyakati tofauti alizituma kwa njia ya M-pesa baadhi ya fedha hizo Sh. 2,500,000, ambapo Sh. 300,000 zilitumwa kwa Flora David Ngowi, Sh. 250,000zilitumwa kwa Agnes Paul Shokolo na Sh. 2,000,000 zilitumwa kwa Omary Mweya Mazanza ikiwa ni sehemu ya fedha za rushwa walizoomba kutoka kwa Masasi.

Washtakiwa walikana makosa yote na kupelekwa rumande baada ya kushindwa kutimiza msharti licha ya dhamana kuwa wazi.

Askari walitakiwa kuwa na wadhamini watatu wa kuaminika wenye barua za utambulisho na nakala za vitambulisho watakaosaini fungu la dhamana ya Sh. 2,000,000 kila mmoja.

Wakala wa M-pesa alitakiwa kupeleka wadhamini watatu wenye barua za utambulisho na nakala za vitambulisho watakaosaini fungu la dhamana Sh. 4,000,000 kila mmoja, hivyo wamepelekwa rumande baada ya kushindwa kukidhi masharti ya dhamana hadi Julai 4, mwaka huu kwa ajili ya kuwasomea maelezo ya awali.
Mpekuzi.

Comments