S.M.Z: Sanaa, Michezo na Utamaduni ni uchumi mkubwa kwa vijana.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (S.M.Z) imejipangia kuifanya Sanaa, Michezo na Utamaduni kuwa ni uchumi mkubwa kwa vijana.

Ili kufikia malengo hayo ni lazima pawepo na ushirikianao mkubwa kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, pamoja na taasisi na watu wengine, jambo ambalo litaleta faida kubwa kwa vijana hao.

Katibu Mkuu Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo Omar Hassan Omar ‘King’ alitoa kauli hiyo katika ukumbi wa skuli ya Haile Salasi wakati akifungua mashindano ya Sanaa ya Maigizo na Uchoraji, kwa mkoa wa Mjini Magharibi yaliyoshirikisha skuli tisa za mkoa huo.
Alisema kuwa kufanya hivyo kutasaidia kwa kiasi kikubwa kuendeleza utamaduni ambapo mikakati maalum imepangwa kulifanikisha jambo hilo, kwa kulifanya jambo hilo kuwa endelevu.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa, Sensa, Filamu na Utamaduni Dk. Omar Abdalla Adam, alisema kuwa mashindano hayo yatafanyika kwa mikoa yote ya Zanzibar, ambapo wameanza na Mkoa wa Mjini Magharibi.

Alisema kuwa mashindano hayo yatafanyika kwa miaezi mitatu na watashirikisha fani ya sanaa ya maigizo na uchoraji, kwa mikoa ya Zanzibar na baadaye kutafuta bingwa wa taifa.

Chanzo: Zanzibarleo

Comments