Aliyasema hayo jana alipokutana na Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya
Mwalimu Nyerere chini ya uongozi wa Mwenyekiti wake, Prof. Mark
Mwandosiya, Ikulu mjini Zanzibar.
Alisema marehemu mzee Karume ana heshima ya pekee kwa Zanzibar na
Tanzania nzima, uamuzi wa chuo hicho kuandaa kongamano hilo ni hatua
moja wapo ya kumuenzi na kumthamini muasisi huyo.
Aliongeza kuwa mzee Karume alikuwa na dira na ndio maana alifanya
mambo mengi makubwa ambayo yataendelea kukumbukwa kutokana na umuhimu
wake.
Alieleza kuwa mzee Karume ndie aliesimamia mapinduzi ya Januari 12,
1964 ambayo yaliwakomboa Wazanzibari na kuwatoa katika unyonge na
hatimae kuondosha ubaguzi wa aina zote.
Aidha, alieleza kuwa kufanyika kwa mapinduzi ni jitihada za mzee
Karume na viongozi wenzake ambapo jitihada hizo zinafaa kuenziwa pamoja
na kutunzwa na kudumishwa ili na vizazi vijavyo viweze kuzifahamu.
Alisema kuwa kuna kila sababu ya kutoa pongezi kwa chuo hicho kwa kwa
hatua hiyo ya kutambua mchango mkubwa wa marehemu Karume ambaye pia, ni
muasisi wa muungano wa Tanganyika na Zanzibar na hatimae kuundwa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Alieleza kuwa marehemu mzee Karume na marehemu Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere waliziunganisha Tanganyika na Zanzibar Aprili 26, 1964
na hadi hivi leo muungano huo umejijengea sifa kubwa ndani na nje ya
Afrika na kuwa wenye manufaa makubwa kwa Watanzania wote.
Sambamba na hayo, alitumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa chuo
hicho kwa kuiimarisha kampasi yake ya Zanzibar ambayo hivi sasa
inasomesha kada mbali mbali sambamba na kuongezeka kwa wanafunzi na
kusisitiza kuwa hiyo yote inatokana na uongozi thabiti uliopo katika
chuo hicho.
Chanzo:zanzibarleo.
Comments