Yanga wazipigia hesabu Sh 600 milioni za CAF.

 WATETEZI wa Ligi Kuu Bara, Yanga imeondolewa katika Ligi ya Mabingwa Afrika, lakini kwa bahati imeangukia Kombe la Shirikisho la sasa inasubiri kujua itacheza na nani, lakini mabeki wake wa kati wameliamsha dude sio mchezo.
Mziki wa Kelvin Yondani na Andrew Vincent 'Dante' umewakuna wana Yanga na kuamini kuwa Sh 600 milioni lazima zitue Jangwani kama tu wataendeleza moto wao hata katika mechi ya mchujo kuwania kuingia makundi ya Shirikisho Afrika.
Yanga ililazimishwa suluhu na Township Rollers ya Botswana baada ya awali kulala nyumbani mabao 2-1, lakini  kiwango walichoonyesha baadhi ya nyota wa timu hiyo imewapa imani baadhi ya nyota wa timu hiyo kuona watavuka salama safari ijayo.
Nahodha wa Yanga, Nadir Haroub 'Cannavaro' aliwasifia wenzake kwa kazi kubwa waliyoifanya Gaborone licha ya safu ya mbele kuwaangusha, lakini akimini kama watajipanga yoyote watakayekutana nao watawanyoosha na kufuzu.
"Kazi nzuri imefanyika katika nafasi ya ulinzi lakini kama tungekuwa na umakini huo katika kufunga tungeweza kufunga kwani tulitengeneza nafasi kadhaa lakini tulishindwa kuzitumia naamini kocha ameliona hilo na atakwenda kulifanyia kazi," alisema Cannavaro, huku  nyota wa zamani wa timu hiyo Edibily Lunyamila na Abeid Mziba wakisema wanaiona Yanga ikitinga makundi kama itacheza kama juzi.
"Ukiangalia kikosi chao msimu huu hata viwango vya wachezaji wao havilingani, ila vijana wameonyesha uwezo wa hali ya juu na kama wangekuwa na matokeo mazuri nyumbani tungekuwa tunazungumza mengine," alisema Mziba.
Lunyamila alisema Yanga ilikuwa wazui katika ulinzi haswa kiwango cha Dante na Yondani na kama watajipanga vema kwa mechi zao zijazo lolote linawezekana na sio ajabu wakitimba makundi kama mwaka 2016.
Katika mwaka huo Yanga ilipenya katika makundi kwa kushinda mechi ya play-offs dhidi ya SD Esperanca ya Angola ambao waliwatungua Dar mabao 2-0 kabla ya kwenda kulala ugenini kwa bao 1-0.

Comments