Wawakilishi, Wabunge tekelezeni ahadi – Sou.


VIONGOZI na watendaji wa majimbo wa mkoa magharibi, wametakiwa kufanya kazi kwa pamoja ili kuendana na kasi ya mabadiliko ya kiutendaji katika kukiimarisha chama chao.

Mwenyekiti wa CCM mkoa huo, Mohammed Rajab Soud, aliyasema hayo katika mkutano wa tathmini kwa ziara yake aliyoifanya hivi karibuni katika majimbo ya mkoa huo kwa ajili ya kukutana na wanachama na viongozi wa chama hicho uliofanyika tawi la CCM Kiembesamaki.

Alisema, umoja, mashirikiano na uzalendo kwa viongozi na wanachama wa chama hicho ndio njia pekee itakayoweza kukimarisha chama na kuendelea kukipatia ushindi.

Aidha, alisema wakati umefika kwa viongozi na watendaji wote wa chama kuachana na fitna, chuki na makundi badala yake wafanye kazi kwa pamoja katika kusimamia na kutekeleza ilani ya chama hicho.

Akizungumzia ahadi zilizotolewa na viongozi wa majimbo, alisema ni jambo la msingi kuhakikisha wanatimiza ahadi hizo kwa haraka ili chama hicho kiendelee kupewa ridhaa na wananchi ya kuendelea kushika dola.

Hata hivyo, alisema uongozi wa mkoa huo umekusudia kuleta mabadiliko makubwa katika kusimamia na kutekeleza ilani ya chama kwa asilimia 100 na kuona wananchi wanapata maendeleo kupitia mambo mbalimbali ikiwemo afya, elimu, miundombinu ya barabara na mambo mengine.

Mjumbe wa Kamati ya siasa ya mkoa, Ayoub Mohammed Mahmoud, alisema CCM tokea enzi za TANU na ASP haiyumbishwi kwani viongozi wake madhubuti kutokana na kuongoza kwa kufuata maadili, katiba na kanuni za chama chao.

Alisema, hivi sasa kuna kazi kubwa ya kufanya katika kuleta mabadiliko ndani ya chama chao kupitia ilani ambayo Makamu  Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein ameitekeleza kwa asilimia kubwa.

Hivyo, aliwasisitiza viongozi hao kushirikiana na wanachama na wananchi wapenda amani na maendeleo kuhakikisha CCM inaendelea kushika dola Zanzibar na Tanzania bara.

Ayoub, ambae pia ni Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi,  akitoa ufafanuzi kuhusu  vifaa vya usafi unaotekelezwa na mabaraza ya vijana, alisema mpango huo upo katika hatua za mwisho kuanza utekelezaji wake ambapo kwa sasa manispaa yanamalizia kuimarisha kanuni.

Kwa upande wao viongozi wa majimbo, walisema ziara ya Mwenyekiti huyo imewaleta pamoja na kubaini kasoro mbali mbali ziliomo majimboni mwao na kuahidi kuzifanyia kazi kwa haraka.
chanzo: zanzibarleo.

Comments