Chirwa? Atazipiga sana tu.

WAKATI watu wanajiuliza ni kwanini benchi la ufundi la Yanga limekuwa likimwamini Mzambia, Obrey Chirwa na kumpa penalti apige licha ya kuzipoteza mara kadhaa, Kocha Msaidizi wa klabu hiyo, Shadrack Nsajigwa, amesema jamaa ataendelea kuzipiga tu.
Nsajigwa amewauliza wanaomsakama Chirwa aliyekosa penalti ya tatu ndani ya mwezi mmoja kuwa mbona anapofunga hakuna anayehoji?
Juzi Jumamosi Chirwa alikosa dhidi ya St. Louis na kuinyima Yanga uongozi wa bao la mapema katika mechi yao ya Ligi ya Mabingwa Afrika, ikiwa ni siku chache tangu akose mkwaju mwingine dhidi ya Ihefu katika Kombe la FA.
Pia mapema mwezi uliopita aliinyima Yanga fursa ya kucheza nusu fainali ya Kombe la Mapinduzi kwa kukosa mkwaju wake dhidi ya URA ya Uganda.
“Mbona hamuulizi amefunga mabao mangapi? Benchi ndilo linalojua nani menye jukumu la kupiga, waacheni wachezaji wafanye yao na tuwaheshimu kwa kazi wanazofanya,” alisema Nsajigwa.


Kauli ya Nsajigwa ni kama ametaka mashabiki na wadau wa soka wote wasiingilie maamuzi yao kwa sababu wanajua wanachokifanya.

Comments