Mahakama ya vileo yawapa onyo wamiliki wa Baa Zanzibar.

Mahakama ya Vileo Zanzibar imewataka wafanyabiashara wa pombe waliopata vibali vya kuendelea na biashara hiyo kwa mwaka 2018  kuzingatia sheria walizopangiwa na serikali na  endapo wataenda kinyume na sheria hizo basi hatua za kisheria zitachukuliwa kwa kufutiwa kibali cha kuuza pombe.

Akizungumza na Zanzibar24 Katibu wa Mahakama ya Vileo Saleh Ali Abdalla amesema licha ya mahakama kujiridhisha vya kutosha katika ukaguzi wa baa zinazofanya biashara hiyo Zanzibar na kuridhia kuwapa  vibali baadhi ya wafanyabiashara  lakini endapo kutatokea uvunjifu wa sheria kwa waendesha biashara hiyo mkono wa sheria utawaadhibu.

Amesema kupewa kibali cha kuuzia biashara ya pombe wamiliki wa baa sio mwanya wa kuwaudhi wananchi kwa kuwafanyia fujo za miziki na kuuza biashara hiyo kiholela kwa watoto chini ya umri.

Mahakama imesema itaendelea kufuatilia Mwenendo wa biashara hizo ili kuondoa malalamiko kwa wananchi na kufuatilia kwa ukaribu mapato ya Serikali yatokanayo na biashara hiyo.

chanzo:Zanzibar24.

Comments