Valery Gerasimov, Mkuu wa Majeshi ya Russia amesema kwa mujibu wa
picha za satalaiti, kambi hizo za kijeshi za Marekani zinatumiwa na
magenge hayo ya kigaidi kutekeleza mashambulizi yao.
Jenerali huyo wa Russia amesema kama tunavyomnukuu: "Hawa ni ISIS tu,
tofauti ni kwamba wamebadili rangi na kujipachika majina mapya kama
'Jeshi Jipya la Syria'. Magenge haya yanatumiwa na Marekani kuvuruga
mambo hususan uthabiti nchini Syria."
Mkuu wa Majeshi ya Russia ameongeza kuwa, Marekani inatumia kambi ya
wakimbizi katika mji wa Al-Shaddadah mkoani Al-Hasakah kaskazini mwa
Syria kama kituo cha kutoa mafunzo ya kijeshi kwa mabaki ya magaidi wa
ISIS.
Amesema kwa sasa kuna takriban magaidi 750 wanaopewa mafunzo ya
kijeshi katika kambi ya kijeshi ya Marekani katika mji wa Al-Shaddadah
huku wengine 350 wakitumia kambi nyingine ya Marekani katika
mashambulizi yake katika mji wa Al-Tanf, katika mpaka wa Syria na
Jordan.
Victor Bondarev, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Baraza
la Shirikisho la Russia ameeleza kuwa Marekani inafanya kila iwezalo ili
kuvuruga tena hali ya mambo huko Syria na kwamba Russia itamsaidia Rais
Bashar al Assad wa nchi hiyo kupambana na suala hilo.
Comments