Russia: Marekani imewapa magaidi kambi zake za kijeshi Syria.

Russia: Marekani imewapa magaidi kambi zake za kijeshi SyriaRussia imesema Marekani inatoa mafunzo ya kijeshi katika kambi zake zilizoko Syria kwa magaidi wakiwemo mabaki ya wanachama wa kundi la kitakfiri la Daesh (ISIS) waliofurushwa eneo la Raqqa.

Valery Gerasimov, Mkuu wa Majeshi ya Russia amesema kwa mujibu wa picha za satalaiti, kambi hizo za kijeshi za Marekani zinatumiwa na magenge hayo ya kigaidi kutekeleza mashambulizi yao.

Jenerali huyo wa Russia amesema kama tunavyomnukuu: "Hawa ni ISIS tu, tofauti ni kwamba wamebadili rangi na kujipachika majina mapya kama 'Jeshi Jipya la Syria'. Magenge haya yanatumiwa na Marekani kuvuruga mambo hususan uthabiti nchini Syria."

Mkuu wa Majeshi ya Russia ameongeza kuwa, Marekani inatumia kambi ya wakimbizi katika mji wa Al-Shaddadah mkoani Al-Hasakah kaskazini mwa Syria kama kituo cha kutoa mafunzo ya kijeshi kwa mabaki ya magaidi wa ISIS.

Amesema kwa sasa kuna takriban magaidi 750 wanaopewa mafunzo ya kijeshi katika kambi ya kijeshi ya Marekani katika mji wa Al-Shaddadah huku wengine 350 wakitumia kambi nyingine ya Marekani katika mashambulizi yake katika mji wa Al-Tanf, katika mpaka wa Syria na Jordan.

Victor Bondarev, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Baraza la Shirikisho la Russia ameeleza kuwa Marekani inafanya kila iwezalo ili kuvuruga tena hali ya mambo huko Syria na kwamba Russia itamsaidia Rais Bashar al Assad wa nchi hiyo kupambana na suala hilo. 
chanzo:parstoday.

Comments