
Hatua hiyo imepingwa na upande wa Katibu Mkuu wa chama hicho Seif
Sharrif Hamad kwa maelezo kuwa chama hicho kwa kushirikiana na vyama
vingine vinavyounda Ukawa vimeshatoa msimamo wa kutoshiriki. Kwa mujibu
wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), uchaguzi katika majimbo hayo ya
Singida Kaskazini, Longido na Songea Mjini utafanyika Januari 13, 2018.
CUF upande wa Profesa Lipumba kupitia kwa Naibu Katibu Mkuu,
Magdalena Sakaya ulisema umewapitisha Delfina Mlelwa kugombea Singida
Kaskazini, Japhary Mneke (Songea Mjini) na Kisiongo Mayasek Olukuya
(Longido).
Naibu Mkurugenzi wa Uchaguzi upande wa Maalim Seif, Shaweji Mketo
alisema hawawatambui wagombea hao walioteuliwa na kupitishwa na NEC. “Wagombea
hawa hawajapitishwa wala kuidhinishwa rasmi na vyombo vyenye mamlaka ya
uteuzi ndani ya CUF na hatutashiriki uchaguzi huu wa marudio,” alisema.
Alisema sababu ya kutoshiriki uchaguzi huo ni kuheshimu na kusimamia
msimamo wa pamoja wa vyama vinavyounda Ukawa vya Chadema, CUF,
NCCR-Mageuzi, NLD na chama mwalikwa Chaumma, uliotolewa baada ya kuibuka
changamoto katika uchaguzi mdogo wa udiwani wa kata 43.
Katika tamko lao la pamoja lililosoma na Mwenyekiti wa Chadema,
Freeman Mbowe, vyama hivyo vilisema kutokana kasoro za uchaguzi huo, NEC
na Serikali walipaswa kukaa mezani kujadiliana na kusitisha uchaguzi
huo ili wadau wakutane kufanya tahmini ya changamoto zilizojitokeza.
Siku tatu zilizopita, Chadema ilikumbana na changamoto inayofanana na
hiyo, lakini ilitokana na mgombea wake kujitosa kuwania ubunge Singida
Kaskazini bila kupitishwa na Kamati Kuu ya chama hicho, hivyo kulazimika
kujitoa.
chanzo: zanzibar24.
Comments