Harakati ya Ansarullah ya Yemen imesema ikilazimu, itaishambulia jamhuri
iliyojitangazia uhuru ya Somaliland kutokana na hatua yake ya
kushirikiana na Umoja wa Falme za Kiarabu dhidi ya wapiganaji wa
harakati hiyo ya Houthi.
Taarifa ya Ansarullah imesema kuwa: "Iwapo Somaliland itatekeleza
azma yake ya kuipa Imarati bandari ya Berbera iitumie katika
mashambulizi yake dhidi yetu, tutajibu mapigo kwa kuvurumisha makombora
ya balestiki dhidi ya eneo hilo lililojitangazia uhuru na mamlaka ya
ndani nchini Somalia."
Mapema mwaka huu, serikali kuu ya Somalia mjini Mogadishu ililaani
hatua ya bunge la Somaliland ya kuafiki mpango wa Imarati wa kutaka
kujenga kambi ya kijeshi katika mji wa Berbera na kuitahadharisha Abu
Dhabi kuwa Somalia itaifungulia mashtaka UAE kwa kukiuka sheria za
kimataifa.
Mpango huo wa Imarati wa kutaka kujenga kambi yake ya kijeshi huko
Somaliland umepingwa na nchi jirani zikiwemo Ethiopia na Djibouti.
Jamhuri ya Somaliland ilijitenga na Somalia mwaka 1991 na kisha kuutangaza mji wa Hargeisa kuwa mji mkuu wake.
chanzo:parstoday.
Comments