SMZ yapewa ushauri wa kutowaacha nyuma wanafunzi wenye ulemavu.

Serikali ya Mapinduzi Zanzibr imetakiwa  kuwasaidia  wanafunzi wenye ulemavu  kuwa  katika  mazingira bora  ya kielimu  yatakayowawezesha  kufaulu  kama wanafunzi  wengine wasio na ulemavu.

Mwakilishi wa Nafasi za wanawake Mwantatu Mbarak Khamis  amesema kutokana na ufaulu  mdogo kwa wanafunzi wenye ulemavu Zanzibar  kunakosababishwa na sababu mbalimbali ipo jana kwa serikali kutafuta mbinu ya kuwasaidia  vijana hao ili kupata elimu itakayowasaidia katika kujenga maisha yao.


Akijibu swali katika kikao cha baraza la wawakilishi Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mmanga Mjengo Mjawiri amesema Serikali  imekuwa  ikifanya  kila njia ili  kuwajengea wanafunzi wenye ulemavu  mazingira bora ya kujifunza ili kuweza kufanya vizuri katika  masomo.

Amesema serikali  imekuwa ikiwasomesha walimu kwa ngazi  mbalimbali  ikiwemo cheti,diploma na kuwajengea  uwezo  ili waweze kuwasaidia watoto wenye mahitaji maalum  kuweza  kujifunza  kupitia elimu mjumuisho pamoja na  kuwapatia vifaa vyote muhimu vya kufundishia.

Aidha Mjengo amesema Wizara yake  itaendelea  na jitihada za kuimarisha  elimu kwa watoto  wenye mahitaji maalum  kwa kuajiri walimu waliohitimu  kozi ya shahada na stashahada ya elimu mjumuisho,Kuweka miundombinu rafiki  kwa watoto  hao ikiwemo ujenzi wa ramps katika skuli 50  unguja na pemba.

chanzo: zanzibar24.

Comments