Mambo yazidi kuwa mambo kwa Tundu Lissu.

Familia ya Mbunge wa Singida Mashariki,Mh. Tundu Lissu imesema kuwa itaweka wazi siku Kaka yao atakapo hamishiwa hospitali nyengine ingawa kwasasa ataendelea kupata matibabu kwenye Hospitali ya Nairobi, Kenya wakati taratibu za kumhamisha zikiendelea.

Vicent Lissu, amesema mbunge huyo atahamishwa kutoka katika hospitali hiyo kwenda kupata matibabu ya kibingwa zaidi kama ilivyoelezwa Jumanne iliyopita na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe.


“Mheshimiwa Lissu bado anaendelea na matibabu kwenye hospitali ileile,” Vicent alisema, “akihamishwa mtajua maana tutaeleza ila kwa sasa bado ni mapema kusema atakwenda nchi gani, itoshe kujua bado yupo Nairobi.”

Hadi jana jioni, dola za Marekani 31,663 (Sh. milioni 69.9) zilikuwa zimechangwa na watu walio ughaibuni kugharamia matibabu ya Lissu, ikiwa ni ongezeko la dola 1,969 (Sh. milioni 4.36) kutoka zilizokuwa zimechangwa wakati Mbowe akizungumza na waandishi wa habari kwa mara ya mwisho jijini Dar es Salaam kuhusu hali ya Lissu.

Kwa mujibu wa mtandao wa www.gofundme.com/Lissumedicalcare, tangu utaratibu huo wa watu walio ughaibuni kumchangia Lissu uanzishwe Septemba 12 na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Vincent Mashinji, mtu aliyetoa mchango mkubwa zaidi ni Yasinta Massawe aliyechangia dola 3,000 (Sh. milioni 6.6).

Mbowe aliwaambia waandishi wa habari Jumanne kuwa michango hiyo imetokana na uhamasishaji unaofanywa na Watanzania walio nje wakiongozwa na Mange Kimambi anayeishi Marekani.

Katika mkutano wake wa Jumanne, Mbowe alisema Lissu ambaye amefanyiwa operesheni 17 hadi Oktoba 12, gharama za matibabu yake zilikuwa zimefikia Sh. milioni 412.45.

“Hata mpaka sasa hivi bado fedha hazijatosha.

“Hapa ninazungumza gharama ya matibabu pekee yake kwa mwezi Septemba zimegharimu fedha za Kenya Sh. 10,687,316 sawa na dola za Marekani 106,875 na ilipofika Oktoba 12 jumla ya gharama ni Sh. 13,708,156 za Kenya.”

Mbowe pia alisema jopo la madaktari 12 ambao walikuwa wanamtibu Lissu wamelipwa Dola za Marekani 46,440 (Sh. milioni 102.5) kwa kuwa kila daktari anapotoa huduma kwa muda fulani anahitajika kulipwa.

chanzo: zanzibar24.

Comments