Sura tatu za Bulembo uchaguzi wa wazazi.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama chaMwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Alhaj Abdallah Bulembo ameonyesha sura tatu katika mchakato wa kuwania tena nafasi hiyo.
Katika sura ya kwanza kwenye mchakato huo Bulembo ambaye ni mbunge wa kuteuliwa, Machi 9, alisema hatagombea tena nafasi hiyo mbele ya kikao cha Baraza la jumuiya hiyo mjini Dodoma. Pia, alitumia fursa hiyo kuwaaga wajumbe akisema hoja si ubunge alioteuliwa, bali ni utamaduni aliojiwekea katika maisha yake.

Sura ya pili ilijionyesha Julai 2, baada ya mwenyekiti huyo kuchukua fomu katika mazingira yaliyodaiwa kuwa na usiri, akieleza kutii shinikizo lililokuwa likitolewa na wazee, viongozi na wanachama wa jumuiya hiyo kumuomba agombea kutetea nafasi yake.
Hata hivyo, akizungumza na waandishi wa habari juzi katika makao makuu ya ofisi hizo, Bulembo aliibuka na sura nyingine akielezea kurejea msimamo wake wa kutogombea na tayari ameshaandika barua aliyoiwasilisha kwa Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana.
“Leo (juzi) nitawasilisha barua yangu kwa katibu mkuu, sitagombea tena ila kwa kuwa bado ni mwenyekiti hadi siku ya uchaguzi nitabakia kwenye kazi ya kusimamia na kuchuja wagombea. 

Awali, nilichukua fomu baada ya kushinikizwa na makatibu wakuu na wazee bwana chukua fomu nikasema tatizo ni fomu tu basi nikachukua,” alisema Bulembo.
Alisema licha ya kuchukua fomu hiyo, bado hakuwapigia simu makatibu hao kuomba msaada kwa kuwa msimamo wake ni kuwapisha wengine waongoze.
Bulembo alisema jumuiya hiyo anaiacha katika hali nzuri akiwa amepunguza deni la Sh4.8 bilioni kwa asilimia 65, kununua pikipiki nchi nzima, kuanzisha mradi wa jengo la ghorofa 14 jijini Dar es Salaam na kumaliza kesi 130. Kuhusu uchaguzi, Bulembo alisema matawi manne kati ya 23,435 bado hayajamalizia uchaguzi, kata 71 kati ya 4,029 hazijamalizia lakini kwa upande wa Zanzibar uchaguzi umekamilika katika majimbo yote 54.

chanzo:mwananchi.

Comments