Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imetakiwa kupunguza tozo ya lesseni ya biashara kwa wafanyabiashara wadogo ili kuwapunguzia gharama kutokana na mitaji yao hailingani na kiwango wanachotozwa na halmashauri.
Akijibu swali katika kikao cha baraza la wawakilishi Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Shamata Shaame Khamis amesema Serikali imezingatia kiwango cha mtaji wa mfanyabiashara na ada ambavyo anatozwa kuwa ipo sawa na haimuathiri mfanyabiashara wowote.
Hata hivyo amesema hakuna tozo kubwa wanaotozwa kwani mfanyabiashara wa kawaida anatozwa kiwango cha Elfu 25 kwa mwezi kwa ajili ya lessen ya biashara na kwa wafanyabiashara wadogo kama mamantilie hutozwa ada ya kuchangia gharama za usafi na si malipo ya lesseni.
Amesema licha ya kuwa serikali imeweka kiwango hicho cha ada kwa wafanyabiashara lakini bado ni kidogo ukilinganisha na gharama zinazotumika katika shughuli mbalimbali hivyo ipo haja ya kuongezwa kwa ada ili kuziongezea halmashauri uwezo na kupunguza utegemezi wa fedha kutoka serikali kuu.
chanzo:zanzibar24.
Comments