DC: Ni msiba mzito kwa Wanampwapwa.



Mkuu wa Wilaya ya Mpwapwa, Jabir ShekimweriMkuu wa Wilaya ya Mpwapwa, Jabir Shekimweri amesema msiba ulioikumba familia ya mbunge wa zamani wa Mpwapwa, Gregory Teu ni mzito kwa wanampwapwa na asingependa kulizungumzia kwa sababu ni la kifamilia.
Alisema kuwa familia ndiyo ilikuwa inakaa kikao cha kujadili taratibu za kusafirisha miili na mazishi na kwamba taarifa kamili itatolewa leo.

Familia ya Teu, ambaye alikuwa Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko imepata msiba mzito kwa kuondokewa na baadhi ya wanafamilia katika ajali iliyoua watu 13 iliyotokea nchini Uganda.
Familia hiyo ilikwenda Uganda kwenye sherehe ya harusi ya ndugu yao na usiku wa Septemba 17, 2017 wakati wakirejea Tanzania, basi lao liligongana na lori katika barabara ya Mataka na kuwaacha watu wanane wakijeruhiwa vibaya.
Kwa mujibu ya taarifa iliyotolewa na kusainiwa na mkurugenzi wa Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais – Ikulu, Gerson Msigwa, Rais John Magufuli ametoa salamu za rambirambi kwa familia hiyo kwa kupoteza wapendwa wao.
“Nimepokea taarifa ya vifo hivi kwa mshtuko mkubwa, nimehuzunishwa na kuondokewa na idadi hii kubwa ya watu, nampa pole Gregory Teu kwa kufikwa na msiba huu mkubwa, nawapa pole wanafamilia, ndugu na jamaa wote walioguswa na vifo hivi.”
“Nawaombea marehemu wote wapumzishwe mahali pema na pia nawaombea majeruhi wote wanaopata matibabu huko nchini Uganda wapone haraka na kurejea nyumbani,” amenukuliwa Rais Magufuli kwenye taarifa hiyo.
Rais Magufuli amewataka wanafamilia wote kuwa na moyo wa subira, uvumilivu na ustahimilivu katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na wapendwa wao na watu muhimu waliowategemea.
Awali, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Augustine Ollomi alisema wanafamilia hao walipata ajali wakiwa kwenye basi aina ya Toyota Coaster lenye namba za usajili za Tanzania ambalo lilikuwa limetokea Uganda kuja nchini. “Ni kweli tumefuatilia basi hilo na kubaini kwamba liliondoka hapa nchini Septemba 15 kwenda Uganda kwenye shughuli ya harusi. Mengine siwezi kusema zaidi mpaka tutakapofanya mawasiliano na mamlaka za Uganda,” alisema Kamanda Ollomi.
Gazeti la Uganda la Daily Monitor limeripoti kwenye tovuti yake kwamba Watanzania hao walikwenda Uganda kwenye harusi ya binti yao, Dk Annette Ibingira ambaye amefunga ndoa na raia wa Uganda, Dk Treasurer Ibingira.
Majeruhi walipelekwa hospitali ya Nkozi kwa ajili ya matibabu lakini baadaye walipewa rufaa na kupelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mulago. Maiti zote zilipelekwa hospitali ya Gombe kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
chanzo:Mwananchi.

Comments