
Balozi wa Cuba Nchini Tanzania Profesa Lucas Domingo Hernandes alitoa
kauli hiyo wakati wa Mazungumzo yake na Makamu wa Pili wa Rais wa
Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi yaliyofanyika kwenye Makaazi yake Mjini
Dar es salaam.
Profesa Lucas Domingo Hernandes alisema mpango huo utahusisha
kuangalia fursa za kuanzishwa kwa mikataba ya Ushirikiano itakayolenga
kuheshimu na kuendeleza uhusiano ulioanzishwa na Waasisi wa Mataifa hayo
Marehemu Fidel Castro wa Cuba na Mwalimu Julius K. Nyerere wa Jamuhuri
ya Muungano wa Tanzania.
Alisema Zanzibar na Cuba ni Visiwa vyenye mazingira yanavyofanana
hasaTamaduni zake kiasi kwamba juhudi za pamoja zinastahiki kuchukuliwa
ili kuona Uchumi, Maendeleo pamoja na maisha ya Wananchi wa pande hizo
mbili yanaendelea kustawi kila wakati.
Profesa Lucas alisema zipo Sekta zilizoleta ufanisi na kuifaidisha
Jamii kwa kiwango kikubwa tokea kuanzishwa kwa ushirikiano wa pande
hizo mbili akitolea mfano ile ya Afya ambayo mafanikio yake
yameshuhudiwa na Wananchi walio wengi.
Balozi wa Cuba Nchini Tanzania alimuhakikishia Makamu wa Pili wa
Rais wa Zanzibar kwamba Cuba itaendelea kuunga Mkono jitihada
zinazochukuliwa na Tanzania na Zanzibar kwa ujumla katika kusaidia
Taaluma kwenye sekta tofauti za Maendeleo.
Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif
Ali Iddi alisema Mpango wa Serikali ya Cuba kupitia Wizara ya Afya
Zanzibar wa kusomesha Madaktari Wazalendo umeleta faraja na kuimarisha
uhusiano wa Nchini Mbili hizo.
Balozi Seif alisema yapo mafanikio makubwa yaliyopatikana katika
Sekta ya Afya tokea kumalizika kwa mafunzo ya awamu ya kwanza ya kundi
kubwa la Madaktari Wazalendo ambapo huduma za matibabu zimezidi
kuimarika katika Hospitali na vituo mbali mbali vya Afya Visiwani
Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimueleza Balozi Lukas kuwa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuimarisha ulinzi wa
Wahadhiri wa Chuo cha Madaktari pamoja na Madaktari wanaotoa huduma za
Matibabu na Taaluma Zanzibar licha ya ishara za vitisho iliyowahi
kujitokeza dhidi ya wataalamu na Madaktari hao.
Othman Khamis Ame
8/7/2017.
chanzo: zanzibar24.
Comments