Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud alisema
muswada wa marekebisho ya sheria ya makosa ya jinai unaotazamiwa
kuwasilishwa mbele ya Baraza la Wawakilishi utawabana watu wanaofanya
suluhu kwa kesi za udhalilishaji wa kijinsia.
Alisema kitendo cha jamii
kuleta suluhu katika kesi za udhalilishaji wa kijinsia kwa kiasi kikubwa
kimechangia kuzorota kwa kesi hizo na wahusika kuwatia hatiani.
Alisema katika marekebisho ya sheria ya mwenendo wa kesi za jinai,
suala la kuleta suluhu katika kesi hizo halikubaliki kwa sababu tayari
kesi za ubakaji ni kosa la jinai.
Akifafanua, alisema jamii imekuwa na
malalamiko mengi kwamba kesi za udhalilishaji wa kijinsia zinakwama
katika ngazi za upelelezi katika Jeshi la Polisi na mahakamani.
Lakini
uchunguzi zaidi umebaini kwamba kesi hizo licha ya kuchukua muda mrefu
katika ngazi ya upelelezi katika jeshi la Polisi lakini jamii imekuwa na
tabia ya kuleta suluhu na kukubaliana na watu waliofanya matukio hayo.
Alisema ni jambo baya zaidi wakati mwingine kesi ya ubakaji
inayomkabili mwanamke, wazazi hukubaliana kwa kuleta suluhu ya kiasi
kidogo cha fedha.
Aidha katika marekebisho ya sheria ya mwenendo wa
makosa ya jinai, suala la dhamana kwa watuhumiwa wa makosa ya
udhalilishaji wa kijinsia ikiwemo ubakaji watanyimwa dhamana.
Alisema
moja ya malalamiko makubwa ya jamii kuhusu mwenendo wa kesi za
udhalilishaji wa kijinsia, ni kwa watuhumiwa wa makosa ya aina hiyo
kupewa dhamana na Jeshi la Polisi na baadaye kuonekana wakizurura
mitaani na kutishia kuvuruga ushahidi ikiwemo kutoa vitisho.
chanzo:Habarileo.
Comments