NMB anzisheni huduma za benki ya kiisalamu Pemba.

nmbUONGOZI wa Benki ya NMB Tanzania, umeshauriwa kuanzisha huduma za kibenki kwa njia ya kiislamu, ikiwa ni hatua ya kuongeza idadi ya wateja, hasa wasiopenda riba, kwenye shughuli zao za kukuza pato lao.

Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa kusini Pemba, Mwanajuma Majid Abdalla, kwenye hutuba yake iliosomwa kwa niaba yake na Katiba Tawala wa Mkoa huo Yussuf Mohamed Ali, mara baada ya kumalizika kwa futari ya pamoja ilioandaliwa na NMB.


Mkuu huyo wa Mkoa, alisema inawezekana wapo wateja wenye imani ya dini ya kiislamu na wengine, wanataka kuingia ndani ya benki hiyo, lakini wanashindwa kwa kuogopa riba, kwenye mchakato wao wa kujiinua kiuchumi.

Hivyo, alisema kama uongozi wa NMB, utaanzisha huduma hizo, inaweza kuwa sababu kwa wananchi kujitokeza kwa wingi ndani ya benki hiyo, sambamba na pato la taifa kukua kila mwaka.

Aidha Mwanajuma alisema, tafiti mbali mbali zinaonyesha kuwa, iwapo taasisi za kifedha zitajenga wigo wa kuwa na dirisha linalotoa huduma za fedha kama mikopo bila ya kuwepo kwa riba, maendeleo zaidi yatapatikana.

“NMB ni chachu ya maendeleo ndani taifa la Tanzania, lakini kama mkianzisha na huduma za kibenki zenye mtazamo wa kiislamu, naamini pato la wateja wenu na la taifa litazidi kupaa”,alifafanua.

Katika hatua nyengine, Mkuu huyo wa Mkoa wa Kusini Pemba Mwanajuma Majid Abdalla, alisema mpango wa NMB kukutana na wateja wao hasa kwenye mkusanyiko wa futari ya pamoja, ni jambo jema linalofaa kuigwa na taasisi nyengine.

“Mkusanyiko huu ni ishara kwamba NMB bila ya kujali itikadi za dini za wateja wao, imekua karibu nao mno jambo ambalo linaamsha ari na nguvu kwa uongozi na watendaji, kutoa huduma bora”,alieleza.

Mapema Mkuu wa kitengo cha Huduma Binafsi za wateja na biashara wa NMB Tanzania Omar Mtiga, alisema NMB imekuwa na utaratibu wa kufutari pamoja na wateja wake, kama njia ya kukutana nao.

“Tayari tumeshafutari pamoja na wateja wetu wa Dar- es Salaam, Unguja, Pemba na kisha Mbeya, Mtwara na mikoa mengine ili kuhakikisha tunakuwa nao pamoja”,alifafanua.

Kwa upande wake Naibu Mufti wa Zanzibar Sheikh Mahamoud Mussa Mawadi, alisema njia ya kufutarishana ni miongoni mwa ibada moja kubwa, hivyo mwenendo kama uliofanya na NMB, uingwe na kila mmoja kwa uwezo wake.

NMB kwa upande wa tawi la kisiwani Pemba, limeshatimiza umri wa miaka 20 sasa, ambapo inaowateja zaidi ya 2000 na ATM tatu ambapo makao makuu yake yapo mjini Chakechake.
chanzo:Mpekuziblog.

Comments