Balozi Seif: Olewao madaktari wanao fanya uzembe wakiwa kazini.

madaktariMakamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi  ameonya kwamba kuanzia sasa Serikali ya Mapinduzi ya Zanziba haitosita kumfukuza kazi mara moja Daktari ye yote atakayebainika kufanya uzembe  wa makusudi bila ya kujali jina au sifa alizonazo Daktari husika.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa onyo hilo wakati akitoa hoja ya kuahirisha Mkutano wa Sita wa Baraza la Tisa la Wawakilishi Zanzibar lililojadili Bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Mwaka 2017/2018 kwenye ukumbi wa Baraza hilo Chukwani nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.


Alisema dhamira ya Serikali kupitia Wizara husika ya Afya ni kutoa huduma bora  yaliyobainishwa na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wakati wakichangia Hotuba ya Wizara ya Afya.

Balozi alisema yapo malalamikombali mbali ya kiutendaji hasa katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja yaliyojitokeza  ambayo huleta kero na maudhi kwa Wananchi wanaofika kupata huduma za matibabu.

Alitanabahisha wazi kwamba  baadhi ya Madaktari wamekuwa na tabia sugu ya kutotekeleza wajibu na majukumu yao wakati wengine wakipenda kutumia lugha chafu zinazowavunja moyo wagonjwa.

Alisema hatua hiyo inakera na kuchukiza Wananchi kutokana na kufikia huduma zinazotolewa kamwe hazilingani na fedha nyingi zinazotolewa na kugharamiwa na Serikali kwa kila Mwezi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alitahadharisha kwamba vipo vifaa kufanyia uchunguzi kwa wagonjwa ambavyo kufanyiwa hujuma kwa makusudi ili wahusika wawaelekeze wagonjwa  kwenda kwenye Hospitali zao au zile wanazopewa baghshishi.

Alisema kitendo hicho kisichokubalika si cha haki kufanyiwa wagonjwa ambao wengi wao ni maskini na baadhi yao hutoka masafa ya mbali kama Vijijini kufuata huduma za matibabu Hospitali za rufaa.
 chanzo:zanzibar24.

Comments