Mkurugenzi Huduma za Ubora wa Maji katika Wizara ya Maji na
Umwagiliaji, Nadhifa Kemikimba aliyasema hayo jijini Dar es Salaam kwa
niaba ya Katibu Mkuu wa wizara hiyo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa
kwanza wa Tanzania na Korea uliokuwa ukijadili teknolojia hiyo ya kutibu
maji.
“Suala la maji safi na salama ni hitaji la msingi kwa kila mwananchi,
kwa hiyo inapotokea teknolojia tunayoweza kuitumia kurahisisha
upatikanaji wa maji safi na salama serikali inakuwa tayari kushirikiana
na yeyote au taasisi yoyote inayoleta teknolojia hiyo,” alieleza.
Aidha, alisema upatikanaji wa maji safi na salama kwa sasa kwa mjini
hakuna changamoto kubwa kutokana na uwekezaji mkubwa uliopo lakini kwa
upande wa vijijini bado kuna changamoto ingawa serikali inajitahidi
kufikia malengo yake.
“Upatikanaji wa maji safi na salama mjini hasa kwa upande wa Dar es
salaam ni asilimia 72 na kwa vijijini ni asilimia 50-65 na tunajitahidi
ili ifikapo 2020 kwa vijijini tuwe na maji safi na salama kwa asilimia
85 na kwa mjini asilimia 95 na mikakati ipo mingi naamini tutafanikiwa”
alisema.
Awali, Balozi wa Korea nchini, Song Geum-Young alisema uhaba wa maji
safi na salama ni changamoto kubwa nchini hasa vijijini licha ya kuwa
kuna vyanzo vikubwa vya maji kama vile maziwa na mito.
Alisema tayari ameshatembelea kwenye baadhi ya mikoa na miji
mbalimbali nchini na kujionea jinsi tatizo la upatikanaji wa maji safi
na salama lilivyokithiri.
Aliongeza kuwa wanatarajia kuanza ujenzi wa mradi wa kusambaza maji
mkoani Dodoma na wameshaanza ujenzi wa mradi wa uhifadhi wa maji taka
jijini Dar es Salaam imbayo ikikamilika itakuwa ni msaada mkubwa kwa
Watanzania.
Kwa upande wake, Rais wa O2 & B Co Limited, SeungHyun Bahn
alisema lengo la mkutano huo ni kujadili namna ya kuboresha na
kuendeleza upatikanaji wa maji safi na salama kupitia miradi ya
kusafisha, kutibu na kuhifadhi maji yatokayo kwenye vyanzo kabla ya
kusambazwa kwa matumizi majumbani.
chanzo:Habarileo.
Comments