Kalemani ampa somo mkandarasi.

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk Medard Kalemani. NAIBU Waziri wa Nishati na Madini, Dk Medard Kalemani amemtaka mkandarasi kutoka Kampuni ya M/s OK Electronics and Electric Limited atakayetekeleza kazi ya kusambaza umeme vijijini awamu ya tatu (REA III) kwa Mkoa wa Shinyanga, kuajiri wananchi wenye sifa kutoka maeneo hayo badala ya kuleta wafanyakazi kutoka mbali.

Alitoa maagizo hayo hivi karibuni katika Kijiji cha Negezi wilayani Kishapu wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III) kwa mkoa huo.


“Tumia wataalamu/vibarua vijana kutoka maeneo haya. Hatutapenda uajiri watu kutoka mbali wakati wafanyakazi wenye sifa wako hapa hapa,” alisema Dk Kalemani na kumwagiza mkandarasi huyo kuhakikisha anawalipa vibarua mara moja kila wanapokamilisha kazi husika. “Hakuna kulaza malipo kwa sababu sisi tunakulipa vizuri,” alieleza.

Sambamba na maagizo hayo, Dk Kalemani aliutaka uongozi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) mkoani humo kujipanga na kumsimamia mkandarasi husika ili kuhakikisha anafanya kazi saa 24 kwa siku.

Alisisitiza kuwa ofisa yeyote atakayelegalega kumsimamia mkandarasi husika kadri inavyotakiwa atawajibishwa kwa kuondolewa katika nafasi yake.

Naibu Waziri pia aliwaelekeza Tanesco kuhakikisha wanawafuata wateja na kuwapatia huduma mahala walipo badala ya kusubiri wateja wawafuate katika ofisi zao, ambazo ni chache na ziko mbali na makazi ya wananchi wengi hususan walioko vijijini.

Kutokana na maelekezo hayo; aliuomba uongozi wa halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Shinyanga, kuanzisha vit uo maalumu ambavyo vitatumiwa na maofisa wa Tanesco kuwahudumia wateja walioko katika maeneo yao.
chanzo:habarileo.

Comments