Temesa yakabidhiwa boti nne za ahadi.

Mtendaji Mkuu wa TEMESA, Dk Mussa Mgwatu MTENDAJI Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Dk Mussa Mgwatu amepokea boti nne zilizokuwa zikijengwa na Kampuni ya Songoro Marine Boatyard ya jijini Mwanza. Amepokea boti hizo jijini humo.

Dk Mgwatu amesema kukamilika kwa boti hizo ni utekelezaji wa ahadi za Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa alizozitoa kwa wananchi wa Pangani mkoani Tanga pamoja na Kilambo na Msangamkuu mkoani Mtwara kwa nyakati tofauti.


Aliongeza kuwa boti hizo nne zitatoa huduma za dharura hasa wakati wa usiku kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa na pia kutoa usafiri mbadala wakati vivuko vikubwa vinapokuwa haviwezi kutoa huduma kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo kupungua kwa kina cha maji katika maeneo ya Kilambo pamoja na Utete mkoani Pwani.

Naye Mkurugenzi kutoka Kampuni ya Songoro Marine Boatyard, Major Songoro alisema boti tatu kati ya nne zilizokabidhiwa zimejengwa kwa kutumia ‘fibre glass’ na boti moja imejengwa kwa kutumia chuma.

Boti ya Mv Kuchele ambayo itapelekwa katika eneo la Msangamkuu Mtwara ina uwezo wa kubeba abiria nane, sawa na boti ya MV Bweni itakayopelekwa Pangani mkoani Tanga.

Mv Mkongo itakayopelekwa Utete, ina uwezo wa kubeba abiria 40 na MV. Tangazo itakayopelekwa Kilambo/Namoto Mtwara ina uwezo wa kubeba abiria 25.

Aidha, Dk Mgwatu aliishukuru serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa kuwezesha ujenzi wa boti hizo na tayari amemuagiza mkandarasi huyo kuhakikisha anazisafirisha boti hizo kwenye maeneo husika haraka iwezekanavyo ili wanachi waanze kunufaika na huduma mbadala itakayotolewa na boti hizo.

Ujenzi wa boti hizo umefanywa kwa kutumia fedha za ndani na umegharimu jumla ya Sh milioni 415.
 chanzo:Habarileo.

Comments