Mfumuko wa bei juu Zanzibar.

Kasi ya mfumuko wa bei imeongezeka kwa asilimia 4.5 katika mwezi wa Februari ikilinganishwa na asilimia 3.7 ya mwezi Januari.

Akizungumza mbele ya waandishi wa habari ofisini kwake Mwanakwerekwe, Mkuu wa kitengo cha bei Ofisi ya Mtakwimu mkuu wa Serikali, Khamis Ahmada Shauri, alisema, kasi hiyo imechangiwa na kuongezeka bei kwa bidhaa za vyakula na zisizokuwa za vyakula.


Alisema, bei za vyakula na zisizokuwa za vyakula zimeongezeka kwa asilimia 4.4 kwa mwezi februari kutoka asilimia 3.5 ya mwezi januari.

Aidha kwa upande wa farisi za bei, ziliongezeka kwa 100.2 mwezi februari ikilinganishwa na 95.6 mwezi januari.

Akizungumzia mfumuko huo, alisema mfumuko huu umekuwepo kwa karibu kipindi cha miezi minne huku akisistiza kuwa hali hiyo inachangiwa na kasi ya bei katika masoko ya bidhaa na nishati.

Nae Meneja Msaidizi Idara ya Uchumi ya Benki Kuu tawi la Zanzibar, Moto Ng’winganele Lugobi, alisema pamoja na mfumuko huo kuongezeka, bado Zanzibar imefikia hatua nzuri kulinganisha na malengo yaliyowekwa ya asilimia 8 kwa nchi za Afrika Mashariki.

“Tunasema ni hali nzuri kwasababu bado tupo bado tupo kwenye tarakimu moja, si hali ya kutisha” alisisitiza.
Alisema Mfumuko wa bei upo kwa karibu nchi zote za Afrika Mashariki ikiwemo Kenya, Uganda, Tanzania Bara na Rwanda. Mfumuko wa bei Tanzania bara umeongezeka kutoka 5.2 mwezi januari hadi kufikia 5.5 mwezi februari, ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 0.3 kiasi ambacho hakina athari katika uchumi wa nchi.
 chanzo:zanzibar24.

Comments