Wagombea wa rika na jinsi mbalimbali waliojitokeza kuchukua na
kurudisha fomu, wamepongeza msimamo huo wa Rais Magufuli ambao umewapa
fursa maskini na matajiri kuingia katika kinyang’anyiro cha kutafuta
tiketi za kuingia EALA.
Msimamo huo wa kuwashughulikia watakaotumia rushwa katika uchaguzi
wowote, Dk Magufuli aliutoa kwenye Mkutano Mkuu Maalumu wa CCM
uliofanyika mjini hapa, Machi 12, mwaka huu, ambako aliahidi
kuwashughulikia wanachama au viongozi watakaotoa au kupokea rushwa
kwenye uchaguzi.
Hadi kufikia jana, wagombea zaidi ya 80 walijitokeza kuchukua fomu
kupitia CCM kuwa wabunge wa EALA katika kituo cha Dodoma, wengine wengi
zaidi ya 200 walichukua Dar es Salaam na wanane wamechukua Zanzibar.
Mwisho wa kuchukua na kurudisha fomu ni leo saa 10.00 jioni.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti wakati wakirudisha
fomu katika chumba cha Katibu Msaidizi Mkuu wa Oganaizesheni Makao Makuu
ya chama jana, walisema ukiachia mbali kuwapo kwa fursa hiyo ndani ya
chama, suala ya kuzuiwa vitendo vya rushwa kumewapa hamasa kuingia
kwenye kinyang’anyiro hicho.
Miongoni mwa waliochukua na kurudisha fomu kuchaguliwa kuwa wabunge
wa EALA ni vijana wasomi na wenye vigezo wanaofika asilimia 50 na nusu
yake ni wasichana.
Uchaguzi huo wa wabunge wa EALA utafanyika Aprili 4, mwaka huu
kuchagua wabunge tisa wa kuiwakilisha Tanzania katika bunge hilo lenye
makao makuu yake Arusha.
Wagombea wote wanatakiwa kufika ofisi ndogo ya Lumumba, kesho wakiwa
na vyeti halisi, baada ya hapo Sekretariati ya Chama Cha Mapinduzi
itahakiki vyeti na majina ya watakaopenya yatapelekwa Kamati Kuu (CC)
itakayokutana siku chache baadaye.
Wagombea watakaopenya kwenye CC , majina yao yatapelekwa mbele ya
wabunge wa CCM na kupigiwa kura watakaoshinda watapelekwa mbele ya Bunge
na kuchaguliwa wabunge sita kutoka chama hicho na kuungana na wapinzani
watatu na kuwa na wawakilishi wa Tanzania tisa katika EALA.
chanzo;Habarileo.
Comments