Bimani: Lipumba hana mamlaka ya kumvua ukatibu Maalim Seif.

bimaniBaada ya Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF), anayetambuliwa na baraza la usajili wa vyama vya siasa, Prof. Ibrahim Lipumba kumvua nafasi ya ukatibu wa chama, Maalim Seif na nafasi kuchukuliwa na Makamu Katibu Mkuu, Magdalena Sakaya, jana Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa CUF Zanzibar, Salum Bimani alisema kuwa katibu wao bado hajaondoka na hajaondolewa kwani Lipumba hana mamlaka hayo.


Akizungumza na kituo cha redio cha Clouds Fm, Bimani amesema mkutano halali unaotambulika ulifanyika Machi, 19 na maamuzi yote yalifanywa kwemye kikao hicho hivyo maamuzi yanayotolewa sasa hayana uhalali.

Aidha msemaji huyo amewataka wanachama wa CUF kutokuwa na hofu na kupuuzia maamuzi yaliyotolewa na Prof. Lipumba na kuwa Maalim Seif atasalia kuwa Katibu Mkuu wa chama kama jinsi ilivyokuwa awali kabla ya kutangazwa kuvuliwa Ukatibu Mkuu.

“Tunapenda kuwambia wanachama wa CUF mkutano walioufanya haukubaliki na hakuna kikao halali kilichofanyika na hata washiriki wake hawakuwa halali … mkutano ulishafanyika na kila kitu kilifanyiwa maamuzi hapo,” amesema Bimani.

chanzo: zanzibar24.

Comments