Kamanda wa
Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Hassan Nassir
alisema jana kwamba watuhumiwa hao ambao hakuwataja, wameanza kuhojiwa na
wamefanyiwa upekuzi kwenye nyumba zao.
“Tunafahamu kuwa
wauza unga ni wajanja kwa kuwa inawezekana wakatupeleka nyumba tofauti na
tuzitakazo, lakini tutahakikisha tunafika maeneo yote ambako tunadhani ni
vichaka vya biashara hiyo,” alisema.
Alisema polisi
haina mpango wa kuwapa taarifa watuhumiwa hao kwa kuwataja majina hadharani na
kwamba kazi inayofanyika ni kuwafuata wanakoishi na kuwapa ujumbe wa kuhitajika
kwa mkuu wa upelelezi kwa ajili ya mahojiano.
Kamanda Nassir
alisema kazi ya kuwahoji watuhumiwa hao ilianza juzi. Kuhusu namna
walivyowatambua, kamanda huyo alisema walipata majina yao kutoka kwa watumiaji
wa dawa hizo.
“Hii ni kazi ya
muda mrefu, tumewatumia watumiaji wa dawa za kulevya katika upelelezi ili
kuwapata,” alisema.
Kamanda huyo
alikana taarifa kwamba kudorora kukamatwa watuhumiwa kunasababishwa na rushwa
ndani ya jeshi hilo kupitia kitengo cha kupambana na dawa za kulevya.
“Pale
tunapowakamata watuhumiwa na baada ya kufanya mahojiano tukiwaachia tunaonekana
tumechukua rushwa, lakini jamii ielewe kuwa hatuwezi kumtia hatiani mtu hadi
ushahidi ukamilike, mkiona hivyo mjue mtu huyo hajaingia moja kwa moja katika
hatia,” alisema.
Alisema vituo
vya Polisi siyo jela, bali ni sehemu ya kufanya uchunguzi wa awali dhidi ya
kesi kwa watuhumiwa, hivyo kuitaka jamii kutofikiria kila mtu anayepelekwa
kituoni ni lazima afungwe au ashtakiwe.
Hivi karibuni,
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Mohamed Aboud Mohamed
alisema Serikali haitamvumilia mtu yeyote ambaye atabainika kuhusika katika
utumiaji, uuzaji, kushirikiana au kuwalinda wahusika wa dawa za kulevya.
Alisema Rais wa
Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein amesharidhia kuwachukulia hatua za kisheria mara
moja wanaobainika kujihusisha na biashara hiyo.
Hatua hiyo ya
Polisi Zanzibar, imekuja siku chache baada ya Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya
Kupambana na Kuzuia Dawa za Kulevya, Rogers Sianga kueleza mipango na mikakati
ya ofisi yake katika kutimiza majukumu yake ambako alisema vita dhidi ya
mihadarati siyo ya Dar es Salaam peke yake, bali ya nchi nzima na kwamba
itafika hadi Zanzibar kwa sababu ikidhibitiwa Bara na ikaendelea visiwani
itakuwa kazi bure.
chanzo:Mwananchi.
Comments