Mikoa mingi yataka kushirikiana na TSN.

BAADA ya Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) kuandaa, kuratibu na kufanikisha Jukwaa la Uchumi katika Mkoa wa Simiyu, baadhi ya mikoa imeonesha nia ya kutaka kushirikiana na kampuni hiyo kuandaa jukwaa kama hilo katika mikoa yao.

Akizungumza na HabariLeo siku moja baada ya kumalizika kwa kongamano hilo, Mhariri Mtendaji wa TSN, Dk Jim Yonazi, alisema ameshapokea maombi kutoka mikoa kadhaa ambayo inahitaji pia kupata jukwaa kama lililofanyika Simiyu Februari 13 mwaka huu.

“Kuna watu wanashangaa kwamba kampuni ya magazeti imefanikiwa vipi kuandaa kitu kama hiki,
lakini sisi tumedhamiria kuandaa mambo mengi zaidi ya haya,” alitamba Dk Yonazi akiwa mwenye furaha baada ya jukwaa hilo la kwanza na la aina yake kufanikiwa kwa kiwango kikubwa.

Dk Yonazi alidokeza, hata hivyo, kwamba mikoa itakayofuata baada ya Simiyu ni pamoja na Dodoma, Arusha, Dar es Salaam na Mwanza.

Kadhalika alidokeza kwamba wadau wengine zaidi wameonesha kutaka kushiriki katika majukwaa yatakayoandaliwa na TSN siku za usoni.

Mhariri huyo Mtendaji alimpongeza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka kwa kuwa mwepesi kukubali kufanyika kwa jukwaa hilo la kwanza mkoani kwake, na kushiriki kikamilifu katika kulifanikisha.

Mapema, Mtaka alielezea kufurahishwa na ujio wa jukwaa hilo mkoani kwake akisema: “Hili ni jukwaa muhimu sana kwetu, jukwaa linalokutanisha taasisi za fedha, Mamlaka ya Mapato, Baraza la Uwekezaji la Taifa na wadau kutoka makundi mbalimbali.Kwa mkoa wa Simiyu ambao tunajenga mabadiliko makubwa ya kiuchumi, hili jukwaa kwetu lina afya sana."

 Wadau wengine waliosaidia kufanikisha jukwaa hilo lililoandaliwa na TSN, wachapishaji wa magazeti ya serikali ya HabariLeo, SpotiLeo na Daily News na kutoa mada mbalimbali ni pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Benki ya NMB, Benki za TIB Development na TIB Corporate na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC).

Kufuatia uwepo wa taasisi hizo muhimu kwa maendeleo, washiriki waliibua hoja lukuki baada ya mada mbalimbali kuwasilishwa ambazo zilisaidia kupata ufahamu katika masuala mbalimbali ya biashara, ulipaji wa kodi na fedha, hususani namna ya kupata mikopo.

Katika jukwaa hilo ambalo ‘mtoto alikuwa hawezi kutumwa dukani’ kutokana na mada motomoto zilizowasilishwa, washiriki walikaa kuanzia saa tatu asubuhi hadi saa mbili usiku bila kuonekana kuchoka.

Mikoa mingi yataka kushirikiana na TSN Mtaka asifiwa kwa kuona mbali TIB: Ibueni fursa mpate mikopo Karibuni kuwekeza Simiyu.

chanzo:Habarileo.

Comments