Hapi: Marufuku nyaraka za ofisi kuhamishiwa nyumbani.

MKUU wa Wilaya ya Kinondoni mkoani Dar es Salaam, Ali Hapi amepiga marufuku viongozi wa mitaa kuhamishia nyaraka za serikali katika nyumba zao binafsi kwa kuwa ni kinyume cha sheria na watakaokaidi watachukuliwa hatua za kisheria.

Agizo hilo la mkuu wa wilaya kwa wenyeviti na watendaji wa mitaa na kata ya wilaya hiyo limekuja baada ya kupata taarifa ya kuwepo kwa mgogoro kuwa katika Mtaa wa Malindi, Kata ya Mbweni uliosababisha kuwepo kwa ofisi mbili moja, ikiwa ni ya serikali na nyingine ikiwa nyumbani kwa Mwenyekiti wa Mtaa huo, Bariki Elibariki.


Hapi alimtaka mwenyekiti huyo na Mtendaji wa Mtaa huo, Abdallah Mkeyenge kukaa chini na kumaliza tofauti zao ambazo kwa sasa zimefikia katika hatua mbaya ya kutoleana lugha za vitisho na kudhalilishana hadharani.

“Hili suala la ofisi ya serikali kuwa nyumbani kwa mtu binafsi haikubaliki hata kidogo na kuna waraka ulitolewa na mkurugenzi kupiga marufuku suala hilo. Nyaraka za serikali haziwezi kukaa kwa mtu binafsi labda kama hiyo ni ofisi yako na mkeo, hilo halituhusu,” alisema Hapi.

Alisema uhusiano mbaya wa viongozi wa mtaa huo yamekuwa yakiwadhalilisha viongozi hao jambo ambalo linawachafulia sifa zao, hivyo waone umuhimu wa kumaliza migogoro yao binafsi.

Amemuagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Suzan Kaganda kufuatilia suala hilo kwa ajili ya kubaini ukweli ili hatua za kisheria zichukuliwe.

“Watendaji ni waajiriwa wa serikali, mwenye mamlaka nao ni Mkurugenzi, Mwenyekiti huna mamlaka ya kumkataa au kumhamisha kwa sababu humtaki, unatoa taarifa kwa mwajiri wake na mkurugenzi ndio anachukua hatua juu yake,” alisema mkuu wa wilaya.

Aliongeza kuwa ana taarifa maeneo mengi ya wazi yameuzwa na watu mbalimbali akiwemo kiongozi mstaafu ambaye hakumtaja, jambo ambalo ni kinyume cha sheria huku akitaka jamii kulinda maeneo hayo.

Awali, akitoa taarifa ya kata, Mtendaji wa Kata ya Mbweni, Kuluthum Msimike alisema kata hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo uhaba wa watendaji wa mitaa ambapo alisema kuna mitaa mitano, lakini watendaji ni wawili.

Msimike alisema katika Mtaa wa Malindi Estate kuna ofisi mbili ambapo moja ni ya serikali na nyingine iko nyumbani kwa mwenyekiti wa mtaa huo, jambo ambalo limekuwa likichangia kudidimia maendeleo ya mtaa huo.

Katika ziara hiyo, Hapi alikagua miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo Shule ya Msingi Kiumbageni, ambako alitoa siku saba kwa ofisi ya Ofisa Elimu wa Manispaa hiyo kuhakikisha anaongeza idadi ya walimu katika shule hiyo na hasa walimu wa awali.

Alisema wilaya hiyo ina ziada ya walimu hivyo ni jambo la ajabu kuona baadhi ya shule zina upungufu wa walimu huku akitaka mwakilishi wa Ofisa Elimu, Fatma Mwiru kuhakikisha anafanya utaratibu wa kuongeza walimu katika shule hiyo.

chanzo:Habarileo.

Comments