Rais Magufuli apongeza HabariLeo kwa kuendeleza amani, utulivu.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye akikata keki pamoja na Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN), Dk Jim Yonazi (kulia kwake), Naibu Mhariri Mtendaji, Tuma Abdallah (kushoto kwake) na Mhariri Mtendaji wa zamani wa TSN, Isaac Mruma (kushoto) kuadhimisha miaka kumi ya kuanzishwa kwa HabariLeo, Dar es Salaam jana. Wanaoshuhudia ni Kaimu Mhariri wa gazeti hili, Nicodemus Ikonko na Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA), Dk Selemani Sewangi. (Picha na Fadhili Akida).RAIS John Magufuli amelipongeza gazeti la HabariLeo na kubainisha kuwa anajivunia kwa kazi nzuri inayofanywa na gazeti hili, hasa katika kuifanya nchi iendelee kuwa na amani na utulivu.

Aidha, gazeti hili limetakiwa kuzibeba ajenda za serikali na kuziwasilisha kwa wananchi, ili wapate taarifa kamili kuhusu utekelezaji wa ajenda hizo, ambazo ni pamoja na viwanda, hali ya utamaduni wa nchi, urithi na sanaa.

Gazeti hili linatolewa na Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) inayochapisha Daily News na Spotileo, ambalo jana liliadhimisha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake Desemba 21, 2006.

Akizungumza wakati wa sherehe hizo, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye alisema alipozungumza na Dk Magufuli asubuhi ya jana kwa njia ya simu kuhusu maadhimisho hayo, Rais alibainisha wazi kuwa anajivunia gazeti hilo kwa kazi nzuri linayofanya.

“Nikiwa njiani wakati nakuja kuhudhuria maadhimisho haya, nilizungumza na mwenye gazeti hili, Rais wetu Dk John Pombe Joseph Magufuli na kumwelezea bayana kuhusu maadhimisho haya. 

Amenipa salamu zake na ameniambia niwaambie kuwa anajivunia sana kazi nzuri inayofanywa na gazeti hili,” Nape alimkariri Rais Magufuli. Alisema Rais ameipongeza timu nzima ya Kampuni ya TSN kwa kumsaidia kuwafanya Watanzania waendelee kuwa na amani. 

“Pia amenituma niwaambie kuwa amepanga kufanya ziara kwenye kampuni yenu, lakini kwa kushtukiza, hakuniambia siku wala saa, jiandaeni,” aliongeza Nape.

Akizungumzia gazeti hili, Nape alisema HabariLeo ni gazeti pekee la Kiswahili la serikali, lililopewa dhamana na jukumu la kuihabarisha jamii kwa kutumia lugha fasaha ya Kiswahili, lakini pia kuwa kiunganishi baina ya serikali na wananchi wake.

“Ujio wa HabariLeo umekuwa na mchango mkubwa sana katika juhudi za kuepuka migawanyiko ya kisiasa nchini, na kuimarisha juhudi za kuendeleza umoja wa kitaifa. 

Hili likiwa ni mojawapo ya malengo ya msingi na kusudio la kuanzishwa kwa gazeti hili na kwa kweli niwapongeze kwa namna mlivyolifanya kwa kiwango cha juu kabisa,” alisisitiza.

Alisema gazeti hilo linaendelea kutoa habari kwa ukweli na uhakika bila kupendelea upande wowote, linaimarisha misingi ya umoja na mshikamano wa Watanzania bila kujali tofauti zao za kiitikadi, kidini, rangi wala kabila.

Nape alibainisha kuwa jambo kubwa na ambalo linaweza lisipatikane katika magazeti mengine ni mtawanyiko wa habari kutoka sehemu mbalimbali za nchi.

“Nikisoma HabariLeo naweza nikapata hata habari za kijijini kwetu, nikapata habari za mbali kabisa tofauti na vyombo vingi ambavyo wakati mwingine unapata habari za mijini peke yake,” alibainisha waziro.

Alilitaka gazeti hili kuhakikisha linabeba ajenda za serikali kama vile suala la kuijenga Tanzania ya viwanda ili wananchi waelewe vyema ajenda hizo na kushiriki katika kuzitekeleza.

“Kwa mfano ajenda ya viwanda, takribani asilimia 80 ya wananchi wanategemea kilimo, katika ajenda hii wanatakiwa kuhabarishwa na kuelimishwa ili washiriki vyema na kunufaika,” alisisitiza, na kuongeza kuwa gazeti hili pia linaweza kuibeba ajenda ya hali ya utamaduni wa Tanzania, urithi na sanaa ili Watanzania waelewe vyema ajenda hizo na kusaidia nchi hiyo isipoteze utamaduni wake.

Alisema anatamani kuiona HabariLeo ya miaka 10 ijayo, inaweza kufika katika maeneo yote nchini na kuangalia namna ya kupenya kwenye taasisi mbalimbali na inamudu ushindani wa soko la kwenye mitandao.

“Mimi kama mteja nisilazimike kubeba nakala halisi ya gazeti lenyewe na hili pengine si mimi tu ninayependa; bali wapo watu wengine wengi wanatamani kusoma HabariLeo kupitia mitandao ya kijamii. 

Najua mmeanza vizuri lakini kuna umuhimu wa kuangalia namna ya kuingiza mitandao mingi zaidi ya kijamii kwa lengo la kuruhusu kufika kwa wateja wenu wengi kwa kuzingatia ukuaji wa teknolijia ya habari na mawasiliano,” alifafanua.

Aidha, Nape aliwataka wafanyakazi wa HabariLeo na TSN kwa ujumla, kuhakikisha wanachapisha habari zenye mwelekeo wa kuona nchi inaendelea kuwa ya amani na utulivu na pia inaendelea kuwa na umoja na mshikamano.

Kwa upande wake, Mhariri Mtendaji wa TSN, Dk Jim Yonazi alisema anashukuru kuwa mmoja wa viongozi wa kampuni ya TSN, anayeshuhudia kutimiza miaka 10 kwa moja ya magazeti ya kampuni hiyo, la HabariLeo, ambalo kwa sasa linatekeleza wajibu wake kama ilivyo lengo la kuanzishwa kwake.

Alisema gazeti hili limejizatiti katika kuwahabarisha wananchi, hasa katika yale wanayoyaelewa na si yale yanayosemwa.

Alisisitiza kuwa kwa sasa gazeti hilo, limeingia katika mkakati wa kuandika habari za kiuchunguzi ili kuisaidia serikali, itambue mambo yanayoendelea, ikiwemo kushiriki katika utungwaji wa sera za serikali.

“Ndio maana msimamo wa HabariLeo umezingatia sana katika kuhimiza maendeleo na kuleta matumaini, limekuwa ni gazeti la kijamii, likijitofautisha na mengine kila inapowezekana,” alisisitiza.

Dk Yonazi alisema gazeti hili, limeongeza wigo wa serikali wa kuwasiliana na watu wake na linatumika kama daraja kati yake na wananchi, kwa kupewa dhamana ya kuhabarisha, kuelimisha, kuburudisha na pia kuhoji mambo mbalimbali ya serikali, katika chama tawala cha CCM na wananchi.

Alitaja kazi za gazeti hili kuwa ni kuanika na kudodosa mambo, yanayofanywa na mamlaka kuelekea uchumi wa kati na kuwasilisha maoni ya wananchi kuhusu mikakati hiyo, hasa Dira ya mwaka 2025 inayoweka wazi vipaumbele vya serikali.

Alisema pamoja na kwamba gazeti hili linakabiliwa na changamoto nyingi, ikiwemo ushindani mkubwa katika soko, mabadiliko ya teknolojia na mabadiliko katika lugha ya Kiswahili, bado linatumia fursa hizo kujipambanua na kuendelea kuhabarisha wananchi.

Alitaja mipango ya kampuni ya TSN katika kujiimarisha zaidi kuwa ni pamoja na kuanzisha huduma ya ushauri huku ikiendelea na huduma yake ya sasa, kuchapisha magazeti ya serikali ya Daily News, Sunday News, HabariLeo, Habari- Leo Jumapili na Spotileo.

Katika maadhimisho hayo, TSN pia ilisaini mkataba na Baraza la Kiswahili Tanzania (BAKITA) wa kushirikiana katika kukuza Kiswahili kupitia HabariLeo.

Mkataba huo ulisainiwa na Dk Jim Yonazi na Katibu Mtendaji wa Bakita, Dk Seleman Sewangi. Akizungumzia mkataba huo, Dk Yonazi alibainisha kuwa TSN imejipanga kupaisha Kiswahili kwa kuhakikisha watanzania wanapata taarifa zilizoandikwa kwa lugha fasaha, lakini pia kuelimishwa juu ya matumizi ya lugha hiyo na baraza hilo.

“Si ajabu kupitia gazeti hili kuchapishwa majarida na vitabu vinvyotumia lugha fasaha ya Kiswahili. Kupitia mkataba huu Bakita watatusahihisha, watatukosoa,” alisema.

Dk Sewangi alisema kupitia mkataba huo, baraza hilo litakuwa linatoa maneno ambayo hutumiwa kwa ufasaha ili kuwajengea uelewa zaidi wananchi kuhusu lugha ya Kiswahili.

Mhariri Mtendaji wa zamani wa TSN, Isaac Mruma alilipongeza gazeti hili kwa kuwa gazeti la kwanza nchini linaloandika kwa kutumia lugha ya Kiswahili na si kutumia lugha ya Kiswahili kuandika.

chanzo;habarileo.

Comments