Algeria yayataka madola ya kigeni yasiingilie masuala ya ndani ya Libya.

Algeria imetoa wito wa kutatuliwa mgogoro wa Libya kupitia njia ya mazungumzo kwa kuyashirikisha makundi na pande zote bila ya uingiliaji wa madola ya kigeni.

Waziri wa Masuala ya Magharibi, Umoja wa Afrika na Umoja wa Ulaya wa Algeria, Abdul Qadir Masahil amesema mgogoro wa Libya unapaswa kutatuliwa kwa njia ya mazungumzo na kwa kuyashirikisha makundi yote yanayozozana nchini humo. Masahil amesema, makundi ya Libya yanaweza kutatua hitilafu zao na kupata suluhisho la matatizo ya nchi hiyo bila ya uingiliaji wa madola ya kigeni.
Amesisitiza kuwa, changamoto kubwa zaidi ya serikali ya umoja wa kitaifa ya Libya ni kukabiliana na ugaidi na kwamba serikali hiyo inapaswa kuungwa mkono na nchi zote jirani na jamii ya kimataifa.
Libya ilitumbukia katika vita vya ndani na baadhi ya maeneo ya nchi hiyo yakadhibitiwa na makundi ya kigaidi baada ya kuondolewa madarakani dikteta wa zamani wa nchi hiyo, Kanali Muammar Gaddafi mwaka 2011. 
Vilevile uingiliaji wa madola ya kigeni hususan Marekani na baadhi ya nchi za Ulaya katika masuala ya ndani ya nchi hiyo umechangia katika kuchochea na kudumisha machafuko nchini humo.     
chanzo:parstoday.

Comments