ZSTC sasa kuuza karafuu soko la Ulaya.

Shirika la Biashara la Taifa Zanzibar (ZSTC) litapatiwa hati ya kuuza karafuu  hai kwenye soko la Ulaya baada ya kutiliana saini na Kampuni ya Ganefryd  ya Denmark  makubaliano ya kuimarisha kilimo hai cha mazao tofauti (organic) kwa kuanzia na kilimo cha karafuu.

Sherehe za kutiliana saini makubaliano hayo zilifanyika katika ofisi za eneo tengefu  Saateni na ZSTC iliwakilishwa na Mkurugenzi Mwendeshaji Dkt. Said Seif na Kampuni ya Genefryd iliwakilishwa na  Afisa  wake Bw. Pale Christeusen.

Akizungumza baada ya kutia saini makubaliano hayo, Dkt. Said amesema Zanzibar  imekuwa ikifanya biashara ya karafuu kwa miaka mingi lakini hivi sasa itapanua wigo wa kuuza karafuu hai Ulaya na kupata faida kubwa.

Alisema Ili Zanzibar iweze kutoa karafuu hai tahadhari kubwa inapaswa kuchukuliwa wakati wa kuotesha miche, ukuaji wake na kufikia wakati wa kuzaa bila ya kuingizwa aina yoyote ya mbolea zenye kemikali.

Ameongeza kuwa uangalizi mkubwa pia unahitaji katika mchakato mzima  wa kushughulika kilimo hicho kuanzia hatua ya  kuchuma, kuanika, kuzihifadhi mpaka kuzisafirisha hivyo amewaomba wananchi  kuunga mkono kuingia katika kilimo hai kwa vile karafuu ndio tegemeo lao na Taifa kwa jumla.

Amesema sambamba na kuanzisha kilimo hai cha zao la karafuu Mkurugenzi Mwendeshaji wa ZSTC amewataka wananchi  kuendeleza zao hilo katika mfumo wa kawaida kwa kuongeza upandaji miche na kuacha tabia ya kukata mikarafuu kwa ajili ya  kuni, kufanyia mkaa na kujengea.

Afisa wa Kampuni ya Genefryd Bw. Pale Christeusen amesema hatua ya kutiliana saini makubaliano hayo ni kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili na kuongeza kipato cha mkulima wa karafuu na kuiongezea Serikali mapato.

Bw. Christeusen amewashauri wakulima wa karafuu Zanzibar kuongeza kilimo hai cha karafuu kwa vile kinafaida kubwa katika soko la Ulaya.

chanzo; zanzibar24.

Comments