Unicef yaipongeza Serikali ya mapinduzi ya Zanzibar kwa huduma za Watoto.

unicefSHIRIKA la Umoja wa Mataifa linalowahudumia Watoto Duniani (UNICEF) limepongeza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika suala zima la kuwahudumia watoto na kuahidi kuendelea kuunga mkono juhudi hizo ili Zanzibar ifikie malengo iliyoyakusudia.

Mwakilishi wa UNICEF katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bi Maniza Zaman aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.

Mwakilishi huyo wa UNICEF hapa nchini alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweza kupata mafanikio makubwa katika kuwahudumia watoto sambamba na kuhakikisha wanapata haki zao za msingi ikiwemo kupata elimu na afya bora.

Alieleza kuwa Shirika hilo linathamini juhudi hizo na limeweza kushuhudia mafanikio na mabadiliko makubwa katika sekta za maendeleo hatua ambazo zimewawezesha watoto wa Zanzibar na wao kuweza kupata haki zao za msingi pamoja na mahitaji yao muhimu ya kimaisha.

Bi Zaman alizipongeza hatua za Serikali ya Mapinduzi za kujenga majengo mapya yatakayowahudumia wanawake na watoto katika hospitali ya Manzi Mmoja na ujenzi wa hospitali mpya ya Abdalla Mazee ni miongoni mwa mafanikio katika sekta ya afya ambayo watoto nao watafaidika.

Vilevile, Mwakilishi huyo alimpongeza Dk. Shein kwa juhudi zake kubwa anazozichukua katika kupiga vita vitendo Ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto kupitia Kampeni aliyoianza mnamo mwaka 2014, kwa ajili ya kukomesha vitendo hivyo.

Alieleza kuwa hatua za Serikali katika kuhakikisha vifo vya akinamama na watoto vinapungua hapa Zanzibar sambamba na kukabiliana na tatizo la mtapiamlo kwa watoto navyo vimepata mafanikio ambapo UNICEF pia, imeahidi kuendelea kuziunga mkono juhudi hizo.

Mwakilishi huyo alieleza kuwa UNICEF tayari imeshaanzisha programu mbali mbali mpya pamoja na kuziendeleza zile za zamani katika suala zima la kuwahudumia watoto na kueleza azma yake ya kwenda ngazi za chini zaidi katika jamii kwa kushirikiana na serikali katika kutatua changamoto zinazowakabili watoto.

Nae Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa upande wake amelipongeza Shirika la UNICEF kwa juhudi zake za kuendelea kuiunga mkono Zanzibar na kuahidi kuimarisha uhusiano na mashirikiano yaliopo.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa Shirika la UNICEF lina historia kubwa na mashirikiano kati yake na Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuimarisha sekta za maendeleo zikiwemo sekta ya afya, elimu sambamba na kuimarisha ustawi wa akinamama na watoto.

Dk. Shein alisema kuwa Shirika hilo limeweza kutoa misaada yake mbalimbali na kuweza kuiunga mkono Zanzibar katika sekta ya afya kwa kushirikiana na Shrika la Afya Duniani (WHO).

Aidha, Dk. Shein amesema kuwa licha ya changamoto kadhaa zinazowakabili watoto katika Bara la Afrika lakini bado Shirika hilo limeendelea kutoa ushirikiano wake na misaada mbali mbali kwa watoto walio ndani ya nchi za bara hilo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza juhudi zilizochukuliwa katika kupambana na vifo vya akinamama na watoto, ambapo Zanzibar imepiga hatua kubwa hasa pale ilipoanzisha mapambano dhidi ya Malaria jambo ambalo limefanikiwa.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo, kutoa pongezi kwa Shirika hilo kwa kuungana na Mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa (UN) yenye Ofisi zake hapa Zanzibar kuunda ‘One UN’ iliozipelekea ofisi hizo kukaa katika jengo moja na kuweza kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.

Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuzisimamia vyema, Sera, Kanuni na Sheria zinazowahusu watoto katika kupata haki zao za msingi na huduma za kijamii.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
chanzo; zanzibar24.

Comments