Makamu wa Rais alitoa agizo hilo katika hotuba yake kwa wananchi na
watendaji wa halmashauri ya Manispaa ya Ilemela waliojitokeza katika
hafla ya uzinduzi jengo la utawala la manispaa hiyo na kukabidhi
madawati 1,074 yaliyotolewa na ofisi ya Bunge.
Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Mawasiliano ya Makamu wa Rais
ilisema, Samia amewataka watendaji hao kuwa karibu na maeneo yao ya kazi
ili waweze kuwa karibu na wananchi na kuwasaidia kutatua kero na
matatizo yanayowakabili kwa haraka.
Akiwa katika wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza wakati anaweka jiwe la
msingi katika mradi wa ukarabati wa machinjio ya Nyakato jijini Mwanza,
Makamu wa Rais aliuagiza uongozi wa jiji la Mwanza kusimamia kikamilifu
mradi wa ukarabati wa machinjio ya Nyakato na kwamba watendaji
watakaobainika kuhujumu mradi ambao utagharimu zaidi ya shilingi bilioni
tatu wachukuliwe hatua kali za kisheria.
Makamu wa Rais alitoa kauli hiyo katika hotuba yake kwa wananchi na
watendaji wa jiji la Mwanza waliohudhuria hafla ya uwekaji jiwe la
msingi katika mradi wa ukarabati wa machinjio ya Nyakato unaohusisha
uboreshaji wa jengo la machinjio, tangi la kuhifadhi maji, ujenzi wa
vyumba vya baridi vya kuhifadhi nyama na ujenzi wa mtambo wa kutibu
majitaka yanayotoka kwenye machinjio hiyo.
Makamu wa Rais pia alimuagiza Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella
kuhakikisha anasimamia uundaji wa menejimenti ya machinjio hiyo ambayo
itaboresha utendaji kazi wa machinjio hiyo.
Kuhusu ukusanyaji wa kodi, Makamu wa Rais aliwahimiza watendaji wa
halmashauri zote za mkoa wa Mwanza kuongeza kasi ya ukusanyaji wa mapato
ya serikali kwa njia ya kielektroniki kutoka kwenye vyanzo mbalimbali
vya fedha ambavyo vitasaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya
wananchi mkoani humo.
Samia alitoa mwito kwa wananchi kuhakikisha wanadai risiti
wanaponunua bidhaa mbalimbali, kwani kufanya hiyo kutasaidia kuongeza
mapato ambayo yataelekezwa kwenye miradi ya maendeleo.
Katika mkutano wake wa majumuisho ya ziara yake ya kikazi ya siku
tano mkoani Mwanza, Makamu wa Rais Samia alisisitiza viongozi na
watendaji wa mkoa wa Mwanza kufanya kazi kwa bidii katika kuwatumikia
wananchi kwa kuzingatia kanuni na taratibu za umma.
Alionya kuwa Serikali ya Awamu ya Tano haitasika kuwachukulia hatua
kali viongozi na watendaji ambao watakwenda kinyume na maadili ya
utumishi wa umma kwenye maeneo yao ya kazi.
Aliwataka viongozi wa mkoa wa Mwanza kusimamia kikamilifu kulinda
hali ya amani na utulivu na wachukue hatua kali kwa watu wanaotaka
kuharibu amani ya nchi.
Makamu wa Rais amehitimisha ziara yake ya kikazi ya siku tano mkoani
Mwanza kwa kukagua, kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi ya
mbalimbali ya maendeleo katika wilaya za Ilemela, Misungwi, Kwimba, Magu
na Nyamagana.
chanzo;habarileo.
Comments