Majibu ya kwanini Uchumi unakua lakini hali za wananchi ni mbaya.

notiKufuatia baadhi ya wananchi kulalamika kuwa hali yao ya kiuchumi inazidi kuwa mbaya licha ya takwimu kuonyesha kwamba pato la taifa linakuwa kwa kasi kila mwaka.

Mhadhiri wa Chuo cha Takwimu cha Afrika Mashariki, Dk. Camillus Kassala amesema sababu inayochangia ukuaji wa pato la taifa kutowiana na hali ya uchumi wa wananchi wengi ni mfumo mbovu wa ugawaji wa pato hilo.

Dk. kassala ameyasema hayo jijini Dar es Salaam katika ufunguzi wa maadhimisho ya siku ya takwimu barani Afrika inayoadhimishwa Novemba 18 kila mwaka.

“Kumekuwepo na mkanganyiko juu ya uwiano wa hali ya kiuchumi ya wananchi na ukuaji wa pato la taifa, itambulike kuwa, pato la kila mwananchi hugawanywa kwa mfumo wa wastani, inachukuliwa pato la taifa linagawaiwa kwa idadi ya wananchi waliopo,” amesema na kuongeza.

“Tatizo linapo anza ni pale serikali inapoligawa, kwamba huligawa maeneo gani na je hayo maeneo hugusa wananchi wengi? Mfano, hugawa kwa njia ya mshahara hivyo wasioajiriwa hawapati, hugawiwa katika mifuko ya hifadhi ya jamii na kwamba wasiokuwepo hawapati gawiwo kwa usawa.”

Amesema kuwa “Mfumo wa ugawaji wa pato la taifa bado una mapungufu ndio maana wananchi wengi wanalalamika kuwa ukuaji wa uchumi wa nchi haushuki kwao na hawafaidiki na pato la taifa ilhali wanakatwa kodi inayokwenda katika pato hilo.”

Kwa mujibu wa takwimu iliyotolewa hivi karibuni na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) inaonyesha kuwa katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka huu pato la taifa limeendelea kukua kwa kasi ya asilimia 7.9 ukilinganisha na kipindi kama hicho mwaka 2015.

Dk. Kassala ameishauri serikali kuwa na takwimu sahihi hususan za wananchi wake na pato la taifa ili kuona namna ya kugawa pato hilo kwa usawa na kufikia wananchi wa kada zote.

chanzo; zanzibar24.

Comments