Hayo yalisemwa Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani juzi na Waziri
Mkuu, Kassim Majaliwa wakati alipotembelea kiwanda cha Equator Suma JKT
kinachojihusisha na uunganishaji magari ya zimamoto na matrekta.
Waziri Mkuu Majaliwa alisema kwa sasa kumekuwa na matukio mengi ya
moto na kusababisha hasara kubwa na majengo au vitu mbalimbali vimekuwa
vikiteketea kabisa kutokana na kukosa magari hayo ambapo yangekuwepo
angalau yangesaidia kupunguza uharibifu.
“Kutokana na kampuni hii kuja na teknolojia ya kisasa ya kuunganisha
magari ya zimamoto moja ya sifa za halmashauri ni kuwa na gari la
zimamoto ambalo litaweza kuwahi kuokoa vitu vinavyoungua ambapo zamani
gharama za zimamoto zilikuwa ni kubwa zinafikia hadi milioni 500 kwa
gari moja hivyo zilishindwa kununua,” alisema Majaliwa.
Alisema mara uzalishaji utakapoanza mwakani magari haya yatashuka bei
kwani gharama itakuwa ni ndogo sana na halmashauri zitaokoa majengo
ambayo yamekuwa yakikumbwa na moto mara kwa mara ikiwa ni pamoja na
shule za sekondari na majengo ya umma.
Kwa upande wa matrekta, alisema asilimia 90 ya Watanzania ni wakulima
hivyo uanzishwaji wa kiwanda hicho kutasaidia upatikanaji wa zana bora
za kisasa za kilimo na matrekta hayo yatapatikana kwa bei nafuu.
Awali, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Equator Suma JKT, Kapteni
Farijala Mkojera akisoma risala ya kiwanda hicho, alisema ujenzi wa
kiwanda hicho ulianza mwaka 2011 na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa
mwaka huu na kuanza uzalishaji Januari mwakani.
Mkojera alisema hadi sasa ujenzi umefikia asilimia 80 ya ujenzi na
gharama hadi sasa ni ziadi ya Sh bilioni moja na kikikamilika
kitagharimu zaidi ya Sh bilioni mbili kitakuwa na uwezo wa kuzalisha
magari 100 na matrekta 3,000 kwa mwaka.
chanzo;habarileo.
Comments